Miongoni mwa Masuala yanayohusu Saumu

  Inamjuzia mfungaji kuonja chakula kwa ulimi wake ili ajue uzuri na ubaya wake (kwa mfano mpisi), kisha akiteme; kwani linalokatazwa ni kukiingiza kooni.

  Atakaekula kwa kudhani kungali usiku, kumbe alfajiri imeshachomoza, kuna kauli kuwa anawajibika kuilipa siku yake hiyo, na kuna kauli kuwa hawajibiki kuilipa na hii ndiyo inayotumika.

   Aliyekula au kunywa akidhania kuwa jua limeshazama, kisha akagundua kuwa bado halijazama, inamlazimu ailipe siku hiyo.

  Atakaechelewesha kulipa saumu mpaka ikafika Ramadhani nyengine, anatakiwa afunge Ramadhani iliyofika kisha alipe siku alizokuwa akidaiwa, na anatakiwa kwa mujibu wa baadhi katika wenye ilmu alishe maskini mmoja kwa kila siku aliyochelewesha kuilipa mpaka ikaingia Ramadhani nyengine bila dharura au sahau.

  Kuingiza dawa kwa tupu ya nyuma k.m. sindano ya nyuma hutengua saumu.

  Kupiga sindano sehemu nyengine hakufungulishi, ila ikiwa inatia chakula mwilini (vitamin).

Kutia dawa ya maji jichoni kunafungulisha ikiwa itafika kooni, na wengine wamesema hakufungulishi. Ama kutia dawa ya maji sikioni hakufungulishi.

   Kutia marham au wanja machoni hakufungulishi, kwani si katika vinavyochuruzika; na kisichochuruzika hakipenyi jichoni kikafika kooni.

  Dawa ya kupuliza anayoitumia mwenye pumu, aki ihitajia mgonjwa katika mchana wa Ramadhani ataitumia kisha atailipa siku hiyo, lakini atajizuia na kula muda uliobaki katika siku aliyotumia dawa. Kulipa kwake ni kuondoa wasiwasi, kwani maulamaa kadha wamemruhusu mfungaji kuitumia bila kulipa saumu yake.  Hukumu hii ikiwa dawa hiyo haihitajii kila siku. Ama akiwa hawezi kuikosa, kila siku lazima aitumie, basi na alishe maskini kwa kila siku ya saumu na anasameheka kufunga.

  Dawa anayofanyiwa mgonjwa wa mafigo (kuosha figo) hufungulisha na analazimika kulipa funga yake baadae.

   Kupimwa damu na kutoa mchango wa damu hakufungulishi.

  Kunyoa nywele za utupuni na kwapani hakufungulishi.

  Mwenye kufunga anaweza kutumia mafuta mazuri.

 Kusati (kuingiza dawa ya mafuta kichwani kupitia puani ili kutibu maradhi ya kichwa n.k.) mchana wa Ramadhani kunahisabiwa katika yanayofunguza; anatakiwa mwenye kufunga aliepuke hilo mchana wa saumu, ila kwa dharura kubwa.

Kutoka damu mdomoni kwa sababu ya kun’goa jino n.k. hakumfungulishi mfungaji ila akiimeza; na kama kumeza huko si kwa makusudi na bila hiari basi hapana neno juu yake na hakutengui saumu.

Aliyefunga akapata mtihani wa kumsaidia mtu asiyejiweza, ikabidi kumuona utupu wake, basi saumu yake haina neno. Kwani hajakusudia.

Atakaemeza makohozi bila kukusudia basi saumu yake haina neno, na atakaeyameza makusudi saumu yake hutenguka.

Moshi wa kujifukiza haufungulishi kuutumia, ila anatakiwa mwenye kufunga auepushe na uso wake, kwani ukiingia kooni kwa makusudi utapelekea kutengua saumu yake.

  Atakaemeza maji anapotia udhu bila kukusudia haharibikiwi na saumu.

Haikatazwi kupiga mswaki mchana wa Ramadhani, bali kunapendelewa, na mfungaji anatakiwa asitumie dawa ya meno isije ikamtangulia kooni.

   Mwanamke anakatazwa kutumia dawa za kuzuia damu ya hedhi ili aweze kufunga; kwani kufanya hivyo si dharura wakati Mwenyezi Mungu amemwekea badala ya kulipa siku za hedhi.

   Kumeza kisicholiwa kunafunguza, ila kukiwa bila hiari.

  Atakaefungua katika Ramadhani kwa udhuru kama maradhi au hedhi au nifasi, anaamrishwa azilipe siku alizokula kwa mfululizo hata kama alifungua katika siku mbali mbali.