UMUHIMU WA KUHUDHURIA VIKAO VYA DINI

Alhamdulilah Rabil Aalamin. Baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu na Kumtakia rehma bwana Mtume Muhammad S.A.W. na kuwatakia radhi Masahaba zake wote na waliowafuata kwa wema hadi siku ya malipo.

Amma Baad:

Katika fadhila kubwa anazozipata Muislamu pale anapokusanyika na wenzake wakasomeshana mambo ya Dini yao na kuelimishana kimaarifa wakapata faida katika kikao chao. Kasema Allah katika Suratil Kahf Aya ya:

اصبر نفسك مع الذين يدعون ربهم بالغداة والعشي يريدون وجهه ولا تعد عيناك عنهم تريد زينة الحياة الدنيا)

(Na isubirishe nafsi yako pamoja na wanaomuomba Mola wao Mlezi asubuhi na jioni, hali ya kuwa wanataka radhi yake. Wala macho yako yasiwaruke kwa kutaka pambo la maisha ya dunia.)

Kwa hivyo wajibu wa kila Muislamu kuhudhuria vikao kama hivi vya kuelimishana mambo ya Dini. Alhamdulilah ndugu zenu wamejitolea kuwaelimisha wenziwao kwa kile walichonacho, wajibu wetu kuhimizana kuja kusoma, kwani kutafuta elimu ni fardhi kwa kila Muislamu kama alivyotueleza Bwana Mtume S.A.W.

Na fadhila kubwa huzipata kila mwenye kuhudhuria  vikao vya elimu, Allah Subhanahu Wataala humpa mja wake zawadi nzuri amabazo hazipatikani katika vikao vyengine. Kasema Mtume S.A.W katika Hadithi iliyotolewa na Imam Muslim.

)وما اجتمع قوم في بيت من بيوت الله يتلون كتاب الله، ويتدارسونه بينهم إلاَّ نزلت عليهم السَّكينة، وغشيتهم الرحمة، وحفتهم الملائكة، وذكرهم الله فيمن عنده (رواه مسلم

(Na hawatakusanyika watu katika nyumba ya Mwenyezi Mungu, wanakisoma  kitabu cha Mwenyezi Mungu, na wanasomeshana baina yao, ila Allah huwateremshia utulivu, na rehma huwafunika na Malaika huwazunguka kwa kuwaombea maghufira, na Allah huwataja waja hawa kwa wema katika Mamlaka yake).  Imetolewa na Imam Muslim.

Ndugu zangu Waislamu, Fadhila kama hizi hazipatikani isipokuwa katika vikao kama hivi vya kuelimishana. Na Muislamu anatakiwa achukue juhudi kubwa katika kujielimisha mambo ya Dini yake.

Orodha ya mambo mema anayotakiwa Muislamu ajilazimu nayo kila siku katika maisha yake:

1- Jitahidi sana kupata Sala zote katika Jamaa, na usikose Takbiratul Ihraraam pamoja na Imam, kwani jambo la kwanza atakaloulizwa mja siku ya Kiama ni Salaa. Na wanawake wasali kila Salaa kwa wakati wake.

2- Jitahidi uzihifadhi sunna za kabliya na baadiya katika kila Salaa.

3- Jitahidi kusoma URADI baada ya kila Salaa na madua ya asubuhi na jioni,     kwani kuna fadhila kubwa katika jambo hilo.

4- Kudumisha ibada ni jambo muhimu, pamoja na kuleta istighfaar na tasbihat za kila aina na kumsalia sana Bwana Mtume S.A.W. kwani kasema:

 (من لزم الاستغفار جعل الله له من كل ضيق مخرجا ومن كل هم فرجا ورزقه من حيث لا يحتسب)

(Atakaedumisha Istighfaar  basi Allah atamuondolea kila dhiki, na kila tatizo atalitatua kisha humruzuku kwa njia asiyoitaraji).

5- Jitahidi sana kusoma Qur`aan kila siku hata kidogo kadiri ya karatasi moja.

6- Jitahidi usali Sala za usiku japo rakaa mbili kabla ya Alfajiri, kwani Sala hii ni nuur katika moyo wako.

7- Kujikurubisha sana kwa Allah, khasa pale unaposimama kufanya ibada, ujidhalilishe kwake na kutaka rehma yake na kumuomba Yeye Pekee.

8- Jitahidi sana kutoa Sadaka na misaada kama una uwezo, kwani Sadaka huondoa balaa. Kama huna cha kutoa basi jikurubishe kwa Allah na vitendo vyengine ili upate ujira sawa na mtoaji sadaka. Mtume kasema: Kutabasamu mbele ya Muislamu mwenzako ni sadaka.

8- Kuwatii wazazi wawili na kuwatembelea jamaa na majirani.

9-Jitahidi uhudhurie darsa na mihadhara, kwani huko ndiko kuuhuisha moyo na kunawiri akili.

10- Jitahidi uwatumikie Waislamu wenzako kwa kuwasaidia kwa kila unaloliweza bila kujikalifisha.

 

Copyright ©2005  Uislam.net