|
Asiyekuwa
kwenye hija atachinja anachotaka kati ya wanyama wa kuchunga wa miguu mine
ili kujikurubisha kwa Allah Aliyetukuka siku ya kuchinja (tarehe 10
Dhul-hija). Imepokewa kwa Bibi Aisha – Mwenyezi Mungu amridhie – kwamba
Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie
- amesema: “Hatafanya mwanaadamu siku ya
kuchinja amali yo yote itakayopendeza mno kwa Allah kuliko kumwaga damu.”
Imepokewa na Tirmidhiy.
Kuchinja siku hiyo ni
sunna iliyotiliwa nguvu; inachukiwa kuiacha pakiwa na uwezo. Dalili ya
kusuniwa ni hadithi aliyoisimulia Muslim kwa sanadi yake kutoka kwa Ummu
Salamah kwamba Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie
- amesema: “Mtakapouona mwezi muandamo
wa Dhul-hija, akataka mmoja wenu kuchinja basi asikate nywele zake na kucha
zake (mpaka achinje).” Imepokewa na Muslim.
Kauli yake [akataka kuchinja] ni dalili ya kusuniwa na sio kuwajibishwa.
YANAYOSHURUTISHWA ILI UDH`HIYA IWE
SAHIHI:
Mnyama anayechinjwa
kutokuwa na ila ya kuchukiza k.m.: chongo wa kubainika, mgonjwa wa kubainika,
na kilema wa kubainika.
Awe kati ya wanyama wa
kuchunga wa miguu mine (ngamia, n`gombe, mbuzi na kondoo).
Achinjwe baada ya sala
ya Idi kwa dalili ya hadithi ya Al-Barau – Allah amridhie – kutoka kwa Mtume
- rehema za Allah na amani zimshukie
- amesema: “La kwanza tunaloanzia katika siku
yetu hii ni tusali kisha turejee tukachinje; atakayefanya hivyo ameipata
sunna yetu; na atakayechinja kabla basi hiyo ni nyama tu amewaletea watu wa
nyumbani kwake, haimo kabisa katika ibada ya kuchinja.”
Imepokewa na Bukhari na Muslim.
Awe amefikia umri
unaokubalika kisharia kama ilivyotangulia
kutajwa kwa mnyama wa hadyi.
MAZINGATIO
Mtu
akichinja kondoo au mbuzi mmoja atamtosheleza yeye na watu wa nyumbani kwake.
Dalili ni hadithi ya Atau bin Yasaar amesema: “Nimemuuliza Abu Ayoub Ansaari
vipi zilikuwa udh`hiya katika zama za Mtume wa Mwenyezi Mungu - rehema za
Allah na amani zimshukie,
akasema: ‘Mtu alikuwa akichinja kondoo au
mbuzi mmoja kwa niaba yake na watu wa nyumbani kwake na wakimla na wakilisha,
mpaka watu waliposhindana kwa ufakhari ndio yakawa kama uonavyo’.”
Imepokewa na Tirmidhiy na akasema ni hadithi sahihi, vilevile imepokewa na
Malik na Ibnu Maajah.
N`gombe au ngamia mmoja hutesheleza kwa
watu saba. Imepokewa kwa Jabir amesema:
“Tumechinja pamoja na Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie - ngamia
mmoja kwa niaba ya watu saba au n`gombe mmoja kwa niaba ya watu saba.”
Imepokewa na Muslim, Abu Daud na Tirmidhiy.
-
Inapendelewa katika mnyama uliyechinja
kula, kutoa sadaka, na kuweka akiba, kutokana na hadithi:
“Kuleni na mulishe na muweke akiba.”
Imepokewa na Muslim.
- Inasuniwa kwa mwenye kujua kuchinja
achinje udh`hiya yake kwa mkono wake mwenyewe, na aseme: “Bismi-LLahi
waLLahu Akbar, Allahumma haadha an fulaan – ajitaje; kwani Mtume wa Mwenyezi
Mungu alichinja kondoo na akasema:
“Bismi-LLahi waLLahu Akbar, Allahumma haadha `anniy, wa `an man lam
yudhah`hi min ummatiy.” (Ewe Allah! kuchinja huku ni kwa niaba yangu na kwa
niaba ya wasiochinja kati ya umma wangu).
Imepokewa na Tirmidhiy na Abu Daud.
Katika adabu za udh`hiya,
mwenye kutaka kuchinja asiondoe kitu kati ya nywele zake wala ngozi yake
wala kucha zake likiingia kumi la mwanzo la mwezi wa Dhul-hija mpaka achinje.
Dalili ya hayo ni hadithi ya Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie
- aliposema: “Likiingia kumi la mwanzo, na ye
yote kati yenu akataka kuchinja, basi asitoe kitu katika nywele zake wala
katika kucha zake mpaka achinje.” Imepokewa na
Muslim; na katika riwaya moja “wala katika
ngozi yake” yaani kwa kunyoa nywele zake za
chini au za kwapani.
Ngozi ya mnyama wa
udh`hiya haiuzwi, lakini inajuzu kuitoa sadaka.
Mchinjaji hapewi sehemu ya nyama ya
udh`hiya iwe ujira, lakini inajuzu kupewa katika nyama hiyo zawadi, kisha
mwenye udh`hiya anaweza kumlipa kwa kazi yake ujira maalumu, kwa dalili ya
hadithi: “Ameniamuru Mtume wa Mwenyezi Mungu
- rehema za Allah na amani zimshukie - nisimamie ngamia na nitoe sadaka
nyama na ngozi yake … na nisimpe mchinjaji kitu kati yake.” Imepokewa
na Bukhari.
Mnyama wa udh`hiya ambae
baada kununuliwa amepata ila inayomfanya asifae kw
udh`hiya, ikiwa mwenyewe
ana uwezo wa kununua mwengine basi ambadilishe; ama akiwa hawezi basi huyo
hutosheleza.
Haitolewi sadaka thamani
ya mnyama wa udh`hiya badala ya kuchinja udh`hiya kwasababu
hilo ni kinyume na sharia. Amesema Aliyetukuka:
)فَصَلِّ
لِرَبِّكَ وَانْحَرْ(
{Basi sali kwa ajili ya Mola wako na
uchinje} [Al-kawthar, 2].
FIDYA
Mwenye
kufanya umra akiona damu kwenye nguo yake baada ya kutokana na ihramu na
hajui wakati gani imeingia hapana kitu juu yake.
Mwenye kulazimika
kuchinja kwa ajili ya fidya asile kitu katika mnyama huyo; akila atachinja
tena.
Atakayevaa
nguo iliyoshonwa au kufunika kichwa chake kabla ya kunyoa au kupunguza
nywele kwa kusahau atalazimika kuchinja kwa ajili ya fidya iwapo atabaki
katika hali hio tangu usiku hadi mchana au tangu mchana hadi usiku. Vilevile
iwapo ataendelea kuvaa baada ya kukumbuka na hakukimbilia kuvua; ama
akikimbilia kuvua basi hapana kitu juu yake.
Mwenye
kuacha kulala Muzdalafa itamlazimu kuchinja, ila ikiwa alibaki Muzdalafa
mpaka kuzama kwa mwezi usiku wa kuamkia siku ya kuchinja.
Mwenye
kuacha kulipiga Jamra la Aqaba atalazimika kuchinja.
Mwenye
kujitoa manii wakati yumo katika ihramu kwa makusudi au amemuingilia mkewe
hija yake au umra yake itaharibika na itamlazimu kuchinja ngamia au n`gombe.
Mwenye
kuacha sai baina Safa na Marwa baada kutufu tawafu ya Ifadha itamlazimu
kuchinja.
Mwenye
kuondoka Mina kabla ya kupindukia jua (adhuhuri) katika siku ya mwanzo ya
kuondoka au ya pili itamlazimu kuchinja.
|