MADHAMBI YA ULIMI

Bismillahi Rrahmani Rrahim. Baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu na kumtakiya rehma Bwana Mtume wetu Muhammad Salla Llahu Alayhi Wasalam na Masahaba zake wote.

Amaa Baad:

Ndugu zangu Waislamu. Assalamu Alaykum Warahamatu Llaahi Taala Wabarakatuhu. Nina furaha kubwa kwa kukutana tena na wasomaji watukufu baada ya kile kitabu kilichopita Marafiki Wabaya, nikaona kuwa bora tuendeleze harakati zetu za kukumbushana katika mema na kupeana nasaha zitakazotufaa katika maisha yetu. Kwani ni wajibu wa kila mmoja wetu kumpa nasaha mwenzake na vile vile ni wajibu wa kila apewaye nasaha njema ni kuikubali tu bila ya kupinga na kukanusha, akajiona kuwe yeye kakamilika wala hana kosa. Japo kuwa hufanyi makosa basi ikubali nasaha hiyo ili upate makumbusho. Kwani sisi Waislamu kila mmoja wetu mbele ya mwenzake ni sawa sawa na kiyoo, yaani  hujiona kama ana makosa pale ambapo anamuona mwenzake anatenda mema, basi na tujaribu kuyatizama maisha ya watu wema ili na sisi tupate kufuata mwendo wao mzuri. Mara nyengine ni uzuri kumuuliza Mtu mwema vipi unaishi maisha yako? Si kwa sababu ya umbea, hasha! Bali kutaka kujuwa mwendo mzuri ili uufuate.

Watu wengi hujipangia maisha yao vile wanavyoyataka wao wenyewe bila ya kujali amri na sheria za Mwenyezi Mungu. Utawaona jambo la kwanza kwao ni kuishibisha nafsi na kuyafuata matamanio yao. Lakini hawajui kwamba Mola wao aliyewaumba kawapangilia mwendo mzuri wa maisha yao ili waishi katika usalama na amani bila ya kudhulumu wala kudhulumiwa. Baada ya hayo akampa kiumbe huyu kila neema zitakazomsaidia kuendeleza maisha yake hapa duniani. Neema ambazo mja huyu akitaka kuzihisabu basi atashindwa wala hataweza kamwe kuzilipa, bali hata katika neema ndogo tu aliyokupa Allah hutoweza kuilipa ewe kiumbe. Basi nini kikudanganyacho ukawacha kumtii Mola wako?

Na katika neema kubwa alizopewa mwanaadamu huyu katika maisha yake ni hii neema ya kuweza kuzungumza ukaeleza nini ulitakalo na ukaweza kuwabainishia watu jema wakalifuata na baya wakaliacha. Huo ni (ULIMI) kiungo kidogo tu! ukikifananisha na vengine, lakini hatari yake kubwa kuliko hivo vengine. Huwenda mtu kutiwa motoni asitoke kwa sababu ya ulimi wake mbaya. Na huwenda ukawa sababu ya kupata radhi za Mwenyezi Mungu katika pepo zake. Viungo vyote vinauwita  ulimi kwa kusema:

( اتَّقِ اللَّهَ فِينَا فَإِنَّكَ إِنِ اسْتَقَمْتَ اسْتَقَمْنَا وَأَنِ اعْوَجَجْتَ اعْوَجَجْنَا )

“Ewe ulimi Mche Mola juu yetu, kwani ukinyooka wewe nasi tutanyooka na ukikaa upande wewe nasi tutakaa upande”.

 Ndio huwenda mtu akasifika mbali kwa sababu ya maneno yake mazuri yenye maana na heshima, na watu wakampa heshima.  Na huwenda mwengine akasifika kwa mbali, kwa ulimi wake ulivyo mbaya hata wengine wakawa wanamkimbia ili kuepukana na maneno yake machafu. Ole wake Mtu kama huyo, tena Ole wake.

Watu wengi wanapuuza sana wayasemayo na wala hawayafikirii, jee ni mema au mabaya, je yanamridhisha Mwenyezi Mungu au Laa. Wao wamo tu, almuradi waseme tu, hawajali kama jema au baya. Hebu tegeni masikio vyema muisikilize Hadithi ya Bwana Mtume (S.A.W) aliyepewa ulimi bora akawafikishia watu wote ujumbe wa Mola Mtukufu. Hadithi ni kisa anakieleza Sahaba mmoja anaitwa Muaadh bni Jabal (Radhi za Mola ziwe juu yake). Hadithi hii imepokelewa na Imam Tirmidhiy na Ibn Majah na Ahmad:

عَنْ مُعَاذِ بْنِ جَبَلٍ قَالَ كُنْتُ مَعَ النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهم عَلَيْهِ وَسَلَّمَ فِي سَفَرٍ فَأَصْبَحْتُ يَوْمًا قَرِيبًا مِنْهُ وَنَحْنُ نَسِيرُ فَقُلْتُ يَا رَسُولَ اللَّهِ أَخْبِرْنِي بِعَمَلٍ يُدْخِلُنِي الْجَنَّةَ وَيُبَاعِدُنِي مِنَ النَّارِ قَالَ لَقَدْ سَأَلْتَ عَظِيمًا وَإِنَّهُ لَيَسِيرٌ عَلَى مَنْ يَسَّرَهُ اللَّهُ عَلَيْهِ تَعْبُدُ اللَّهَ لَا تُشْرِكُ بِهِ شَيْئًا وَتُقِيمُ الصَّلَاةَ وَتُؤْتِي الزَّكَاةَ وَتَصُومُ رَمَضَانَ وَتَحُجَّ الْبَيْتَ ثُـمَّ

قَالَ أَلَا أَدُلُّكَ عَلَى أَبْوَابِ الْخَيْرِ الصَّوْمُ جُنَّةٌ وَالصَّدَقَةُ تُطْفِئُ الْخَطِيئَةَ كَمَا يُطْفِئُ النَّارَ الْمَاءُ وَصَلَاةُ الرَّجُلِ مِنْ جَوْفِ اللَّيْلِ ثُمَّ قَرَأَ: (تَتَجَافَى جُنُوبُهُمْ عَنِ الْمَضَاجِعِ ) حَتَّى بَلَغَ ( جَزَاءً بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ) ثُمَّ قَالَ أَلَا أُخْبِرُكَ بِرَأْسِ الْأَمْرِ وَعَمُودِهِ وَذُرْوَةِ سَنَامِهِ الْجِهَادُ ، ثُمَّ قَالَ أَلَا أُخْبِرُكَ بِمِلَاكِ ذَلِكَ كُلِّهِ قُلْتُ بَلَى فَأَخَذَ بِلِسَانِهِ فَقَالَ تَكُفُّ عَلَيْكَ هَذَا قُلْتُ يَا نَبِيَّ اللَّهِ وَإِنَّا لَمُؤَاخَذُونَ بِمَا نَتَكَلَّمُ بِهِ قَالَ ثَكِلَتْكَ أُمُّكَ يَا مُعَاذُ وَهَلْ يُكِبُّ النَّاسَ عَلَى وُجُوهِهِمْ فِي النَّارِ إِلَّا حَصَائِدُ أَلْسِنَتِهِمْ )

Maana yake:

          “Kutoka kwa Muaadh bni Jabal kasema kwamba; nilikuwa safarini pamoja na Bwana Mtume (S.A.W) nikaamka siku moja karibu naye tukawa tunakwenda, nikasema: Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu. Niambie amali gani nifanye ili iniingize Peponi na iniepushe na Moto. Mtume (S.A.W) akasema: Umeuliza jambo kubwa, nalo ni jepesi kwa yule aliyorahisishiwa na Mwenyezi Mungu. Umuabudu Mwenyezi Mungu na wala usimshirikishe na kitu. Na usimamishe Sala na utowe Zaka na ufunge Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na uwende Kuhiji Nyumba ya Mwenyezi Mungu. Kisha Mtume akaendelea kusema: Je nikufundishe milango ya kheri? Saumu ni kinga na Sadaka huzima moto wa dhambi (hufuta) kama maji yanavouzima moto, na Sala ya mtu pinga pinga la usiku, Kisha Mtume (S.A.W) akasoma Aya (Huiniuka mbavu zao kutoka vitandani wakati wa usiku ili kumuabudu Mola wao….) mpaka akafika Aya isemayo (Hayo ni malipo ya yale waliyokuwa wakiyafanya) Surat Sajdah Aya 16 – 17.

Kisha Mtume (S.A.W) akasema: Jee nikwambie jambo kubwa kuliko yote hayo; ni (Jihadi). Kisha akasema tena: Je nikwambiye kinachotawala yote hayo yaliyopita? Muaadh akasema: ndio niambie, Mtume (S.A.W) akachukuwa ncha ya ulimi wake na kusema: Jiepushe na huu (ulimi). Muaadh akamuuliza Mtume (S.A.W) Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu. Kwani sisi tunahisabiwa kwa kila tunayoyasema? Mtume (S.A.W) akashangaa na kusema: (Thakilatka Ummuk) yaani ole wako! Kwani hawatomiminwa watu katika Moto  isipokuwa kwa ncha za ndimi zao.” Yaani kwa sababu ya madhambi ya ulimi ndio watu watatumbukizwa katika moto. 

Wallahi Hadithi hii ni muhimu sana kila mmoja wetu kuijuwa, wanaume na wanawake, wadogo na wakubwa. Ili kila mmoja awe anatahadhari sana na kuchuma madhambi ya ulimi bila yeye kujuwa. Na inatutosha onyo kali kutoka kwa Mtume (S.A.W) pale aliposema katika Hadithi sahihi iliyopokelewa na Imam Al Bukhary na wengineo:

( مَنْ كَانَ يُؤْمِنُ بِاللَّهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ فَلْيَقُلْ خَيْرًا أَوْ لِيَصْمُتْ )

Maana yake:

          “Mwenye Kumuamini Mwenyezi Mungu na kuiamini siku ya Mwisho basi aseme la kheri au anyamaze kimya”.

Na kumbuka kwamba neno unapolitamka tu, basi kuna Malaika tayari wanaliandika katika daftari lako. Kasema Mwenyezi Mungu katika Surat Qaaf Aya ya (18):

( مَا يَلْفِظُ مِنْ قَوْلٍ إِلَّا لَدَيْهِ رَقِيبٌ عَتِيدٌ )

Maana yake:

          “Hatoi mtu kauli yoyote isipokuwa karibu naye yuko mngojeaji tayari (kuandika).

Basi kwa nini ewe mja ulijaze daftari lako kwa mabaya ambayo ulikuwa ukiyachuma mwenyewe kwa ulimi wako. Ulikuwa ukiwachekesha wenzako kwa kusema uwongo ili usifiwe. Jee Wako wapi leo? Mbona hawakusaidii lolote, wewe ndie mwenye kukhasirika. Soma kwa makini Hadithi ya Mtume pale anapomtahadharisha msema uwongo mwenye kuwafurahisha wenzake vikaoni. Kasema Mtume (S.A.W) katika Hadithi iliyotolewa na Imam Tirmidhy na Abi Daud na Imam Ahmad:

(وَيْلٌ لِلَّذِي يُحَدِّثُ بِالْحَدِيثِ لِيُضْحِكَ بِهِ الْقَوْمَ فَيَكْذِبُ وَيْلٌ لَهُ وَيْلٌ لَهُ)

Maana yake:

          “Ole wake mwenye kuhadithia hadithi ili awachekeshe watu na huku akisema uwongo. Ole wake tena Ole wake”

Hatari kubwa hiyo. Lazima watu watahadhari na wazichunge ndimi zao ili wajiokowe na adhabu kali ya Mwenyezi Mungu. Tunamuomba Allah atuwezeshe kusema kila la haki na la kheri na kuwacha maneno ya upuuzi (Amin).

 

Copyright ©2005  Uislam.net