KUTUFU NA KUSAII

 

Ni kuizunguka Kaaba kuanzia kwenye Jiwe Jeusi na kumalizia hapo hapo ili utimie mzunguko wa mwanzo, na hurudiwa mara saba pamoja na kutamka “SubhaanaLLah walhamduliLLah, walaa ilaaha illa-LLah waLLahu akbar” na kuomba dua.

VIPI KUTUFU:

* Tawafu huanza kwa kulibusu Jiwe Jeusi ikiwezekana; isipowezekana atatosheka na kuligusa au kuliashiria kwa mkono wake pamoja na kutamka “Allahu Akbar” wakati wa kulishika.[1]

è    Ataanza kutufu na hali ameifanya Nyumba ya Allah iwe kushotoni kwake.

è   Ataomba dua atakazo wakati wa kutufu na atasoma “Albaaqiyaatu-ssaalihaatu” yaani “SubhaanaLLah walhamduliLLah, walaa ilaaha illa-LLah waLLahu akbar”

è  Anapokuwa sawa na Pembe ya Yamani ataigusa ikiwezekana na hataiashiria kama hakuweza kuigusa.

è    Akifika kwenye Jiwe Jeusi mzunguko wa kwanza unakuwa umemaliza, na atanza mzunguko wa pili kama alivyofanya mwanzo mpaka atimize mizunguko saba.


[1] - Inasuniwa kukabir katika kila mzunguko hata katika mzunguko wa mwisho, na akitamka “BISMILLAHI” kabla yake itakuwa vizuri kwa vile hilo limepokewa kutoka kwa Ibnu Umar – Allah amridhie – kwamba alikuwa anapolishika Jiwe hilo husema: “BISMILLAHI WALLAHU AKBAR”. Ameipokea Baihaqiy na wameisahihisha jumla ya wenye ilmu.

SUNNA ZA TAWAFU:

1.    “Ramal”: Nayo ni kutembea kwa haraka na hatua zinazokaribiana bila kwenda mbio na kuchupa; hili linasuniwa katika mizunguko mitatu ya mwanzo.

2.     “Idh-tiba`u”: Nayo ni kupitisha sehemu ya kati ya shuka anayojifunika chini ya bega la kulia kwenye kwapa na kuzitupia ncha zake juu ya bega lake la kushoto, yaani aweke wazi bega lake la kulia. “Idh-tiba`u” huwa katika mizunguko yote saba.

Tanbihi: “Ramal” na “Idh-tiba`u” haziwi ila katika tawafu ya “quduum” tu (tawafu ya mwanzo akifika Maka).

3.    Rakaa mbili za tawafu: Nazo ni rakaa mbili zinazosaliwa nyuma ya Maqam ya Nabii Ibraahim - amani imshukie - au po pote itapowezekana baada ya tawafu. Dalili ya hilo ni hadithi ya Ibnu Umar Allah amridhie iliyoko kwa Bukhari anasema: Alikuja Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie - akaizunguka Nyumba ya Allah mara saba kisha akasali nyuma ya Maqam rakaa mbili kisha akatoka kwenda kwenye Safa, na Allah Aliyetukuka amesema:

) لَقَدْ كَانَ لَكُمْ فِي رَسُولِ اللَّهِ أُسْوَةٌ حَسَنَةٌ(

{Bila shaka katika Mtume wa Allah mmekuwa na kigezo kizuri} [Al-ahzaab 21].

MAZINGATIO

¨   Mwenye kutufu akawa na shaka katika idadi ya mizunguko aliyozunguka ataendelea kutoka idadi iliyo ndogo kati ya idadi mbili anazozifikiria, na akiirudia upya tawafu baadae ni vyema.

¨  Mwenye kuingia manukato anapoligusa Jiwe Jeusi na Pembe ya Yamani bila kukusudia kupata mabaki ya manukato hayo humo itampasa ayaoshe mwilini na hakitamlazimu kitu kingine.

¨   “Ramal” kama ilivyo kwa wajao Maka kutoka nje vilevile huwa kwa wakaazi wa Maka.

¨  Inajuzu kusali rakaa mbili za tawafu baada ya sala ya alfajiri kabla ya kuchomoza jua na baada ya sala ya alasiri kabla ya kuchwa jua kwa kauli iliyopewa uzito na wenye ilmu, kwasababu hiyo ni sala yenye sababu iwapo atatufu katika nyakati mbili hizi.

¨  Rakaa mbili za tawafu huakhirishwa iwapo ni wakati usioruhusiwa kusali, nao ni nyakati za kuchomoza jua, kuchwa jua na kuwa katikati ya mbingu kwa jua katika kipindi cha joto kali isipokuwa siku ya Ijumaa.

¨   Inajuzu kutufu Nyumba Takatifu wakati imamu anahutubu Ijumaa lakini bora kusubiri.

¨  Mtu asitufu kwenye tabaka ya pili ya jengo ila isipowezekana kutufu kwenye tabaka ya chini.

¨  Haimlazimu mwenye kutufu kuvua viatu vyake na anaruhusiwa kuvichukua mkononi au chini ya kwapa vikiwa nadhifu.

¨ Haitakiwi kutufu juu ya sakafu ya Msikiti - yaani tabaka ya juu kabisa – kwasababu hawi katika usawa na Nyumba Takatifu.

¨  Haijuzu kutufu ndani ya ule ukuta mfupi wa “alhatiim” kwasababu ni sehemu ya Kaaba.

¨  Inajuzu kwa mwenye kuhiji au kufanya umra anapotufu au anaposai kupumzika katika ibada hizo akihitaji hilo.

¨  Akitufu au kusai akaongeza mzunguko mmoja au miwili bila kukusudia hapana kosa juu yake lakini inapendelewa arudie upya ili kuondoa wasi wasi.

 

KUSAI BAINA SAFA NA MARWA

1.       Akikaribia kwenye Safa atasoma kauli Yake Aliyetukuka:

) إِنَّ الصَّفَا وَالْمَرْوَةَ مِن شَعَآئِرِ اللّهِ(

{Hakika Safa na Marwa ni katika alama za kuadhimisha dini ya mwenyezi Mungu} [Albaqara, 158].

2.    Atapanda juu yake mpaka aione Nyumba Takatifu, atakabir mara tatu kisha atamhimidi Allah, na anapendelewa aseme mara tatu:

"لا إله إلا الله وحده لا شريك له ، له الملك وله الحمد وهو على كل شيء قدير، لا إله إلا الله وحده ، أَنْجزَ وعده ونَصَرَ عبده ، وهزمَ الأحزابَ وحده"

“Laa ilaaha il-la-llaahu wa`hdahu laa shariika lahu, lahul-mulku walahul-`hamdu wa huwa `alaa kulli shay’in Qadiir. Laa ilaaha il-la-llaahu wa`hdah, anjaza wa`adah, wa nasara a`bdah, wa hazamal-a`hzaaba wa`hdah”

(Hapana anayestahiki kuabudiwa ila Allah peke Yake hana mshirika. Ufalme ni wake na Yeye ndiye wa kushukuriwa na Muweza juu ya kila kitu. Hapana anayestahiki kuabudiwa ila Allah peke Yake. Ametimiza ahadi Yake, akamnusuru mja Wake na akayashinda makundi ya washirikina peke Yake).

Kisha ataomba dua atakazo.

3.       Kisha atashuka kuelekea Marwa huku anamdhukuru Allah Mtukufu, mpaka akifika baina ya alama mbili za rangi ya kijani atatembea kwa haraka zaidi, na anapendelewa aseme:

"رب اغفر وارحم، إنك أنتَ الأعزُّ الأكرم"

“Rabbi-ghfir war-`ham, innaka antal-aa`z-zul-akram”

(Mola wangu samehe na urehemu; hakika Wewe ndiye Mwenye uwezo mkuu na ukarimu wa juu).

Wanawake haiwapasi kutembea kwa haraka.

4.   Kisha atatembea taratibu huku anamdhukuru Allah na kumuomba kheri ya duniani na ya akhera mpaka akikaribia Marwa atasimama juu yake na kufanya kama alivyofanya juu ya Safa, na kwa hayo atakuwa ameshamaliza duru moja.

5.   Kisha atafanya duru ya pili kutoka Marwa hadi safa na atafanya kama alivyofanya katika duru ya mwanzo mpaka atimize duru saba kwa kumalizia kwenye marwa.

6.   Inajuzu kusai pasina tohara lakini anapendelewa awe katika tohara.

MASHARTI YA SAI:

1)      Iwe baada ya tawafu.

2)      Iwe duru saba.

3)      Ianzie kwenye Safa, imalizie kwenye Marwa.

 

MAZINGATIO:

v   Wanazuoni wamehitalifiana kuhusu hukumu ya sai: kuna kauli ni fardhi na kuna kauli ni sunna. Kwa kauli ya kwanza, atakayeiacha basi hija yake hubatilika, na kwa kauli ya pili hija yake haibatiliki lakini atawajibika kuchinja, nayo ndiyo kauli ya wengi wa wanazuoni wa Madhehebu hii.

v    Mwenye kusai kuanzia marwa na kumalizia Safa kisha akatokana na ihramu itamlazimu arejee kwenye ihramu yake na atimize sai yake kwa kutoihisabu duru ya mwanzo ambayo alianzia Marwa hadi Safa, kisha atawajibika kuchinja mara mbili.

v   Haikatazwi kusai upande mmoja kutoka Safa hadi Marwa kwenda na kurudi, kwani ugawaji wa eneo la sai ni kwa ajili ya kuwepesisha, jambo ambalo halikuwapo hapo kabla, lakini bora kufuata nidhamu ya mwendo iliyowekwa ili kuondoa msongamano.

v   Mwenye kusai chini ya duru saba na hakukumbuka ila baada ya kutokana na ihramu itampasa arejee ihramu yake na atimize sai yake kisha itamwajibikia kuchinja.

v   Kupanda juu ya vilima viwili vya Safa na Marwa kunasuniwa kwa wanaume kwa kadri ya mmoja wao kuiona Kaaba sio kwa wanawake.

v   Iwapo mwenye kusai hakuweza kuisoma dhikri iliyopokewa juu ya vilima viwili vya safa na Marwa haikatazwi kwake kuisoma wakati anapotembea baina yake.

 

KUTOKANA NA IHRAMU YA UMRA:

·    Akimaliza mwenye kufanya umra sai yake atanyoa au kupunguza nywele zake. Kunyoa ni bora kuliko kupunguza, na izingatiwe kwamba kupunguza lazima kuenee kichwa chote.

·     Baada ya kunyoa au kupunguza nywele atakuwa ameshatokana na ihramu yake akiwa mfanya Tamat-tuu. Ama akiwa mfanya Qiraanu hatanyoa ila siku ya kuchinja kule Mina.

·    Yanamhalalikia mwenye kufanya umra baada ya kutokana na ihramu kila yanayomharamikia muhrimu isipokuwa kuwinda katika Eneo Takatifu (Al-Haram).

·    Mfanya Tamat-tuu bora kwake kupunguza nywele baada ya kufanya umra, na kunyoa baada ya kulipiga Jamra Kuu la Aqaba na kuchinja ikiwa nywele zake fupi baina ya umra na hija.

 

MAZINGATIO:

¡    Mwenye kuhirimia hija au umra kisha akavaa nguo iliyoshonwa baada ya kukamilisha ibada hizo lakini kabla ya kunyoa au kupunguza nywele atalazimika kuchinja.

¡     Hakatazwi mtu kujinyoa au kujipunguza nywele mwenyewe kwa ajili ya kutokana na ihramu, lakini inachukiwa kufanya hivyo uchukivu wa kiutakaso akiwapo wa kumfanyia hayo kati ya wasio wahirimu.

¡     Hazuiwi muhrimu kumnyoa au kumpunguza nywele muhrimu mwengine, kwani hapana dalili ya kuzuia, na kuzuia hili kutaleta usumbufu mkubwa, lakini bora yule ambaye ameshatokana na ihramu amtoe katika ihramu aliye muhrimu.

¡     Mwenye kutanguliza kunyoa kabla ya kuchinja na kupiga Jamra, kuna kauli kuwa atayefanya hivyo kwa sahau au kutokujua hana kosa, na kauli hii ndiyo inayofuatwa katika fatwa, na kuna kauli kuwa atayefanya lo lote kati ya hayo atalazimika kuchinja.

¡     Haisihi kwa mfanya Tamat-tuu kutokana na ihramu yake ya hija kabla ya kuchinja mnyama wake. Ikiwa hakuweza kuchinja siku ya kuchinja (10 Dhulhija) atabaki na ihramu yake mpaka achinje.

¡      Halitoshi wanalofanya wengi kati ya watu zama hizi - la kukata nywele kidogo kwa mwanamme, bali wajibu kupunguza sehemu zote za nywele mpaka ijulikane kuwa mtu huyo amepunguza nywele zake.

 

 

Copyright ©2004  Uislam.net