KUTOKANA NA IHRAM YA HAJ NA UMRA

 

Akimaliza mwenye kuhiji siku ya kuchinja (10 Dhulhija) kupiga jamra na kuchinja atatokana na ihramu yake kwa kunyoa au kupunguza nywele. Dalili ya hayo ni hadithi ya Anas “kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu - rehema za Allah na amani zimshukie - alifika Mina akaja kwenye Jamra akalipiga kisha akenda alikofikia katika Mina akachinja, kisha akamwambia kinyozi: ‘Ondoa’, akaonyesha upande wake wa kulia wa kichwa kisha wa kushoto.” Imepokewa na Muslim na Ahmad.

 Mwanamke haruhusiwi kunyoa kwa ajili ya umra wala hija, bali anapunguza kadiri ya inchi moja. Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie - amesema: “Na linalowapasa wanawake ni kupunguza tu nywele zao.” Imepokewa na Abu Daud.

 Kunyoa ni bora kuliko kupunguza, kwasababu Mwenyezi Mungu amekutaja mwanzo katika kauli Yake Aliyetukuka:

) مُحَلِّقِينَ رُؤُوسَكُمْ وَمُقَصِّرِينَ(

   {mkinyoa vichwa vyenu na mkipunguza nywele} [Al-fat`h, 27], na kwasababu Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie - amesema: “Allah awarehemu wenye kunyoa” mara tatu, pakasemwa: ‘na wenye kupunguza?’, akasema: “Na wenye kupunguza.” Imepokewa na Rabiu, Bukhari na Muslim.

   Yanamhalalikia mwenye kuhiji baada kunyoa (au kupunguza) yale yote aliyozuiliwa kwasababu ya ihramu isipokuwa mke na kuwinda. Hali hii huitwa “tahal-lul as-ghar” yaani kutokana na ihramu kudogo. Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie - amesema: “Mkishapiga jamra na kunyoa itakuwa halali kweni kila kitu ila wake zenu.” Imepokewa na Nasaaiy, Ahmed na Baihaqiy.

TAWAFU YA IFADHA NA SAI

  Tawafu ya ifadha ni moja kati ya nguzo za hija; hija huharibika kwa kuiacha.

  Ni katika sunna kutekeleza mawili haya siku ya tarehe 10 Dhul-hija baada ya kupiga jamra, kuchinja na kunyoa au kupunguza nywele, lakini inajuzu kuyaakhirisha japo baada ya siku za tashriq.

  Mwenye hedhi ataakhirisha tawafu ya ifadha mpaka atahirike.

Baada ya kutekeleza mawili haya inakuwa halali kwa mwenye kuhiji kila alichokuwa kazuiliwa isipokuwa kuwinda kwenye eneo la Haram; na hali hii huitwa “tahal-lul akbar” yaani kutokana na ihramu kukubwa.

 

    MATANGAZIO:

  Atakayetufu tawafu ya ifadha kisha akalala Maka mchana na kurejea Mina jioni hapana kitu juu yake lakini amefanya kinyume na lililo bora.

 -  Haizuiwi kula na kunywa Maka baada ya tawafu ya ifadha, ila imekataliwa kulala hapo mchana, lakini linalotegemewa katika fatwa ni kuwa inajuzu kulala mchana kwa vile imethibiti kuwa Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie - alilala mchana baada ya kutufu.

-   Aliyetufu tawafu ya ifadha mizunguko sita akakumbuka baada ya kurejea nchini kwake itamlazimu arudi kwenye Haram na arudie tawafu ya ufadha katika mwaka wake huo, na hapana kitu juu yake kwa rai ya baadhi ya wanazuoni ikiwa hajamuingilia mkewe; ama ikiwa vinginevyo basi hana budi kuhiji tena.

 

 

 

Copyright ©2004  Uislam.net