FADHILA ZA KUMI LA MWISHO

Assalaamu 'alaykum warahmatullah wabarakaatuh

Wapenzi Waslamu:

Alhamdulilal tunamshukuru Allah aliyetuwezesha kuifunga Saumu ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa wakati uliopita, Na hivi sasa waislamu wanalisubiri kwa hamu fadhila za kumi la mwisho la mwezi huu, siku kumi ambazo hupatika ndani yake kheri nyingi, ndani yake kuna usiku ambao ni bora kuliko ibada za miezi elfu, (miaka 83).

Kasema Allah katika Suratil Qadr:

(إنا أنزلناه في ليلة القدر ، وما أدراك ما ليلة القدر، ليلة القدر خير من ألف شهر، تنزل الملائكة والروح فيها بإذن ربهم من كل أمر، سلام هي حتى مطلع الفجر)

(Hakika Sisi tumeiteremsha Qur'ani katika Laylatul Qadri, Usiku wa Cheo Kitukufu * Na nini kitacho kujuulisha nini Laylatul Qadri? * Laylatul Qadri ni bora kuliko miezi elfu. * Huteremka Malaika na Roho katika usiku huo kwa idhini ya Mola wao Mlezi kwa kila jambo. * Amani usiku huo mpaka mapambazuko ya alfajiri).

Ndio maana bwana Mtume (S.A.W) akatufundisha suna moja muhimu, ambayo hivi sasa watu wengi sana wameiacha, nayo ni suna ya (Itikafu) kulazimu msikiti na kukaa ndani yake muda wa hizi siku kumi ili kupata fadhila, kuacha kulala sana na kula sana na kuwaacha watoto kidogo kwa ajili ya Alla subhanahu wataala, kwa kutaka kupata fadhila za usiku huu mtukufu wa (LAYLATUL QADR).

Muislamu akijitahidi kufanya ibada katika usiku huu, kwa kusali sana na kusoma kuraan na kumdhukuru Allah na kufanya vitendo vingeni vya kheri kama kuwalisha masikini na kuwatazama wanaohitaji katika waislamu wenzake, basi huwenda akapata fadhila za usiku huu, bila kuona ishara zozote zile kama wanavyoitakidi watu wengi ya kuwa lazima eti uone taa inameremeta kama karabai au uone maajabu fulani, Maneno haya yote hayana dalili sahihi kuwa lazima yatokezee hayo, wewe amka tu na ufanye ibada na Allah ndie mwenye kujua siri ya usiku huu.

Ndio maana siku yake maalumu ikafichwa asiijuwe mtu, hata Bwana Mtume S.A.W alibainishiwa wakati wake, lakini hakuchukuwa muda hapo hapo akaisahau, kwa maana tunatakiwa kujitahidi katika zile siku muki zote za mwisho katika Mwezi huu mtukufu wa Ramadhani.

Imepokelewa kutoka kwa Mtume S.A.W hadithi isemayo:

من قام ليلة القدر إيمانا غفر له ما تقدم من ذنبه

"Atakae simama usiku wa Laylatul Qadr kwa kufanya ibada kwa imani kamili, basi hufutiwa madhambi yake yote yaliyotangulia,"

Na tuchukue mfano mzuri kwa bwana wetu S.A.W katika kutenda ibada, alikuwa S.A.W zikifika siku za kumi la mwisho basi hujitayarisha na kuingia msikitini kwa niya ya Itikafu, na kufanya ibada. Mama Aisha Radhi za Allah ziwe juu yake alimuuliza Mtume S.A.W dua gani nzuri kusoma katika usiku huu, akamjibu sema:

اللهم انك عفو تحب العفو فاعف عني

Waislamu, hii ni fursa kubwa kwa kila mwenye kutaka kujikurubisha kwa Mola wake, ni njia pekee ambayo humsaidia kila mwenye kutaka kurudi kwa Mwenyezi Mungu. Hujuwi kama utaishi mpaka mwakani ili uweze kufunga tena, kwa nini tunachelewesha tawba.