KUCHINJA

 

Baada kulipiga Jamra la Aqaba mwenye kuhiji atachinja mnyama wake wa hadyi ili kumfuata Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie.

  Kinachochinjwa huwa ngamia au n`gombe au kondoo au mbuzi. Kondoo au mbuzi mmoja hutosheleza kwa mtu mmoja ikiwa ametimiza mwaka, na kuna kauli miaka miwili. N`gombe akiingia mwaka wa nne na ngamia akiingia mwaka wa sita hutosheleza kwa watu saba.

ö     Kuchinja kuliko wajibu huwa kwa mfanya-tamat-tuu na mfanya-qiraanu.

ö     Mnyama huyo huchinjwa ndani ya eneo la Haram.

ö     Inapendelewa amchinje mwenye kuhiji mwenyewe akiweza.

ö     Anapendelewa ale sehemu ya nyama yake na atoe sadaka iliyobaki.

ö     Mfanya-ifraadu hawajibiki kuchinja.

 

MAZINGATIO:

  Iwapo amenunua mnyama wa kuchinja na kwa ajili ya msongamano hakutowa thamani basi haitamwajibikia kumrudisha, lakini atapaswa  ikiwa hamjui mwenyewe aigawe thamani yake kwa mafakiri.

  Haimjuzii mwenye kuhiji kununua mnyama wa kuchinja kwa njia ya Benki ya Kiislamu kwasababu kutokana na ihramu kwa mfanya-tamat-tuu kunategemea kuchinja, naye hajui wakati gani atachinjiwa, na kutokana na shaka ya hilo.

  Haijuzu kumchinja mnyama wa hadyi kabla wakati wake na vilevile haijuzu pasipo mahali pake. Wakati wake ni siku ya kuchinja (10 Dhul-hija) na kwa hiyo atakaechinja kabla yake basi na achinje tena.

   Asipoweza mwenye kuhiji kuchinja siku ya kuchinja atabaki na ihramu yake mpaka achinje kwasababu haisihi kutokana na ihramu kabla kuchinja.

  Asiyeweza kumpata mnyama wa hadyi itampasa afunge siku ya tarehe: sita, saba, na nane Dhul-hija kisha afunge siku saba baada kumaliza amali za hija.

  Inajuzu kuchinja mnyama wa hadyi katika sehemu zote za Haram na sio eneo la Mina pekee kwani hii ni kauli ya baadhi ya wanazuoni tu.

   Haijuzu kupewa nyama mchinjaji kwa ajili ya uchinjaji bali ampe ujira wake mbali.

  Mwenye kufanya umra katika miezi ya hija kisha akarudi nchini kwake na akaazimia kuhiji kwa ifraadu (kufanya hija pekee) haitamlazimu kuchinja kwasababu ya kutokuwa katika hukumu ya mfanya-tamat-tuu.

  KUTOKANA NA IHRAMU YA HIJA

    Akimaliza mwenye kuhiji siku ya kuchinja (10 Dhulhija) kupiga jamra na kuchinja atatokana na ihramu yake kwa kunyoa au kupunguza nywele. Dalili ya hayo ni hadithi ya Anas “kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu - rehema za Allah na amani zimshukie - alifika Mina akaja kwenye Jamra akalipiga kisha akenda alikofikia katika Mina akachinja, kisha akamwambia kinyozi: ‘Ondoa’, akaonyesha upande wake wa kulia wa kichwa kisha wa kushoto.” Imepokewa na Muslim na Ahmad.

    Mwanamke haruhusiwi kunyoa kwa ajili ya umra wala hija, bali anapunguza kadiri ya inchi moja. Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie - amesema: “Na linalowapasa wanawake ni kupunguza tu nywele zao.” Imepokewa na Abu Daud.

     Kunyoa ni bora kuliko kupunguza, kwasababu Mwenyezi Mungu amekutaja mwanzo katika kauli Yake Aliyetukuka:

) مُحَلِّقِينَ رُؤُوسَكُمْ وَمُقَصِّرِينَ(

   {mkinyoa vichwa vyenu na mkipunguza nywele} [Al-fat`h, 27], na kwasababu Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie - amesema: “Allah awarehemu wenye kunyoa” mara tatu, pakasemwa: ‘na wenye kupunguza?’, akasema: “Na wenye kupunguza.” Imepokewa na Rabiu, Bukhari na Muslim.

     Yanamhalalikia mwenye kuhiji baada kunyoa (au kupunguza) yale yote aliyozuiliwa kwasababu ya ihramu isipokuwa mke na kuwinda. Hali hii huitwa “tahal-lul as-ghar” yaani kutokana na ihramu kudogo. Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie - amesema: “Mkishapiga jamra na kunyoa itakuwa halali kweni kila kitu ila wake zenu.” Imepokewa na Nasaaiy, Ahmed na Baihaqiy.

 

 

 

Copyright ©2004  Uislamu.net