HUKUMU ZA SIKU YA 8 DHUL-HIJA (MINA)

 

  Mfanya hija ya qiraanu au ifraadu ataelekea Mina na ihramu yake, na mfanya tamattuu atahirimia hija pahala alipofikia au po pote katika eneo la Haram.

  Kukithirisha talbia na dua wakati wa kuelekea na anapokuwapo huko Mina .

  Mwenye kuhiji atasali Mina sala zote tano yaani adhuhuri, alasiri, magharibi, isha na alfajiri ya siku ya tarehe 9 kwa kupunguza rakaa za sala ya rakaa nne, kutokana na hadithi iliyothibiti kutoka kwa Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie: “kwamba alitoka kwenda Mina siku ya Tarwiya (8 Dhul-hija) akasali huko sala tano.” Imepokewa kwa maafikiano. Bora kusali kila sala kwa wakati wake.

  Kuwapo Mina usiku wa kuamkia tarehe 9 Dhul-hija ni sunna iliyowajibika; atakaelala kwengineko itamlazimu kuchinja, ila akiwa katika wenye udhuru hatawajibikiwa na kitu, lakini amekosa ujira mkubwa. Dalili ya hili ni hadithi ya Urwa bin Mudharris amesema: “Nimekuja kwa Mtume - rehema za Allah na amani zimshukie - nikamwambia nimekujia kutoka Milima miwili ya Tay-i, nimekichokesha kipando changu na kuitaabisha nafsi yangu; hakuna mlima wo wote ila nimesimama juu yake, je basi, nitakuwa nina hija? Akasema: Mwenye kusali nasi sala ya alfajiri hapa na hali alifika Arafa kabla ya hapo atakuwa amesharuhusiwa kujisafisha na hija yake imetimia.” Imepokewa na Ahmed na Wenye sunan na akaisahihisha Tirmidhiy.

 

     MAZINGATIO:

 

  Inasihi kwa aliyehirimia hija kwenda Mina siku ya Tarwiya (8 Dhul-hija) asubuhi au baada ya jua kupindukia (adhuhuri); kinachosuniwa kwake ni kusali sala tano zote huko Mina.

  Hakuzuiwi kutangulia kuhirimia hija kabla siku ya Tarwiya (8 Dhul-hija), vilevile hakuzuiwi kulala Mina usiku wa kuamkia siku ya Tarwiya, lakini sunna ni vile ilivyotangulia kutajwa.

 

 

 

 

Copyright ©2004  Uislam.net