HUKUMU ZA SIKU YA 10 DHUL-HIJA

 

  Ataondoka Muzdalafa kabla kuchomoza jua kuelekea Mina.

  Akifika mwenye kuhiji Mina ataanza kwa kulipiga Jamra la Aqaba, ambalo linaitwa Al-Jamratu L-kubra (jamra kuu).

  Kupiga jamra kunakuwa kwa vijiwe vidogo kama punje ya dengu, na huwa kwa vijiwe saba.

 

VIPI KUPIGA JAMRA:

ý     Jamra la Aqaba hupigwa kutokea ndani ya bonde liliopo hapo kwa kuifanya Maka iwe kushotoni na Mina kuliani, kijiwe kimoja kimoja mpaka vitimie vijiwe saba pamoja na kukabir kwa kila kijiwe. Imepokewa kutoka kwa Jabir: “Kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu - rehema za Allah na amani zimshukie - alikuwa akikabir kwa kila kijiwe.” Imepokewa na Muslim.

ý     Wakati wa kulipiga jamra hili huwa baada ya kuchomoza jua siku ya idi hadi kupindukia jua (adhuhuri).

ý    Inaruhusiwa kupiga jamra hili hadi kuchwa kwa jua la siku ya idi kwa dharura na kwa wenye udhuru.

ý     Mwenye kuhiji atasita kutamka talbia akitupa kijiwe cha kwanza kulipigia jamra la Aqaba, kutokana na hadithi ya Al-fadhlu ibnu Abbaas: “Niliendelea kumsikia - rehema za Allah na amani zimshukie - akitamka talbia mpaka akalipiga Jamra la Aqaba.” Imepokewa na Rabiu.

 

   MAZINGATIO:

  Kupiga Jamra la Aqaba ni siku ya mwanzo ya kuchinja (10 Dhul-hija) kuanzia baada kuchomoza jua na kuendelea, na kupiga jamra zote tatu ni katika siku za Tashriq kuanzia kupindukia kwa jua (adhuhuri) na kuendelea.

  Haitoshelezi kuvifunga vijiwe kwenye mfuko na kuvirembea bali lazima kila kijiwe kitupwe peke yake.

  Hakuna ubaya kwa mwenye kuhiji kumwakilisha mtu mwengine ampigie jamra anaposhindwa kufanya hilo mwenyewe.

  Ni lazima kuhakikisha kuwa vijiwe vinavyorembewa vimelipata jamra, vinginevyo atakuwa katika hukumu ya asiyepiga, na imeruhusiwa kwa dharura iwapo vimeangukia kwenye hodhi la jamra.

 

 

Copyright ©2004  Uislam.net