|
Haijuzu
kwa mwanamke kwenda hija au umra bila mahramu. Ikiwa hakupata mahramu wa
kufuatana naye ameruhusiwa kusafiri kwa ajili ya hija ya fardhi pamoja na
watu wema wanaofuatana na wake zao au wanawake walio mahramu zao.
Mwanamke akipata hedhi
kabla kutufu tawafu ya umra naye amenuia kuhiji kwa kutanguliza umra kabla
hija (tamat-tuu) na hakutoharika kabla siku ya tarwiya (8 Dhul-hija),
atabadili siku hiyo nia yake anuie kuchanganya hija na umra (qiraanu)
- aingize hija kwenye umra, na itamtosha tawafu moja na sai moja kwa hija na
umra yake.
Masharti
ya hija kwa mwanamke hayatafautiani na masharti ya hija kwa mwanamme;
anachozidi mwanamke ni sharti moja tu, nayo ni kuwa afuatane na mumewe au
mahramu yake kwa ajili ya uharamu wa kusafiri peke yake.
Mwanamke
mwenye kuhiji haimlazimu kusali katika Misikiti Miwili Mitukufu (wa Maka na
wa Madina); hilo linapendelewa kwake iwapo
ataepuka msongamano na wanaume na hatakuwa katika hali inayoogopewa
mshawishiko. Yakikosekana masharti mawili haya kwake basi sala yake ni
katika nyumba aliyomo.
Kubadilisha nguo kwa
mwanamke hakuathiri ihramu yake.
Ziara
ya makaburi ya Masahaba na ya Watu wa nyumba ya Mtume - rehema za Allah na
amani zimshukie - ni jambo lenye hitilafu; na
kujuzu kwa hilo ni kwa sharti ziara iwe kwa ajili ya mazingatio ya mauti na
isiwe na kilio cha sauti wala mengineyo katika yaliyokatazwa.
Haijuzu
kwa mwanamke kufunika uso wake; akiufunika makusudi itamlazimu kuchinja; na
ikiwa kwa kukosea au kusahau itampasa ajifunue haraka akikumbuka. Vilevile
anazuiwa kuvaa glavu mikononi.
Mwanamke
inamwajibikia kupunguza katika ncha za nywele zake wakati wa kutokana na
ihramu kadiri ya upana wa vidole viwili, na kuna kauli kadiri ya upana wa
vidole vinne. Asipofanya akatokana na ihramu bila
hilo itamlazimu kuchinja.
Inamjuzia mwanamke
kumwajiri mtu ampigie vijiwe jamra ikibidi.
Inamjuzia mwanamke
kutumia vidonge vya kuzuia hedhi kwa ajili ya dharura ya kuhiji au kufanya
umra.
Mwanamke
akipata habari ya kifo cha mumewe akiwa kwenye hija itamwajibikia kutimiza
ibada za hija yake na haimjuzii kuiacha baada ya kuwa kishahirimia.
|