BIBI YUKABID

               MAMA YAKE NABII MUUSAAA (A.S)

 

æóÞóÇáóÊú ÇãúÑóÃóÉõ ÝöÑúÚóæúäó ÞõÑøóÉõ Úóíúäò áöí æóáóßó áóÇ ÊóÞúÊõáõæåõ ÚóÓóì Ãóäú íóäÝóÚóäóÇ Ãóæú äóÊøóÎöÐóåõ æóáóÏðÇ æóåõãú áóÇ íóÔúÚõÑõæäó(9) ( ÇáÞÕÕ : 9)

 Qurratu `Ainin lii Wa Laka, Laa Taqtuluunhu  `Asaa an yanfa`anaa aw Nattakhidhahu waladan. (Surat L- Qasas : 9 ).

 Firauni * alizindukana kimkumkum na usingizi ukamruka akaa macho hadi mchana kweupe kuzim hakuna nyota. Hapo asubuhi akapiga mbiyo ya mgambo, kwa Firauni kuna mambo, watakiwa makohani wa majini na ng`ambo, wote wafike hapo wakasikiye mambo.

Kukakutanika makohani pamoja na wachawi na waganga wakubwa wote kwa Firauni. Aliwayeleza kuwa yeye kawota ndoto mbaya bila ya kiyasi hata hakupata usingizi tena, ukamruka wala asijuwe ulipokwenda. Sasa kawayita hapa ili wamfasiriye maana ya ndoto yake hiyo. Baada ya kuchemsha mbongo walimuweleza kuwa atazaliwa mwana wa kiyume katika Bani Israaiil (Yahudi), ambaye ndiye atakayekuwa sababu ya mauti yake Firauni. Mtoto huyo atamnyang`anya Firauni ufalme wake na nguvu zake zote asaliye hohe hahe, hana mbele hana nyuma. Si hayo tu bali piya atamtowa katika ardhi hii yeye pamoja na watu wake. Na hata dini hatayiyachiliya ila atayibadilisha na ataleta dini nyengine. Alipouliza zama aw wakati wa kuzaliwa mtoto huyo, alijibiwa kuwa hayo ni mambo yaliyofichika hawawezi katu kuyajuwa. Kusikiya haya Firauni zilimpanda pomoni na akawa ni mwingi wa wasi wasi. Alifinyangika hapo, na mwisho akatowa amri ya kuuwawa kila mtoto wa kiyume anayezaliwa na tumbo la Bani Israaiil. Piya alijaza masikiyo na maaskari waliowalaliya dago wana wa Israaiil, hata ilikuwa wenyewe Bani Israaiil wakiziyogopa zile nguwo zawo wenyewe wanazozivaa, licha watu. Wengi kati ya hawo majasusi hasa walikuwa wakunga na wazalishaji wapitawo majumbani ili kuzalisha ; kwani wawo ndiwo hasa wanaoweza kujuwa nchi kadha nani kazaa mtoto gani. Bila ya shaka na maaskari wengine piya walikuwemo kazini.

Jitihada hayiondowi kudura. Alizaliwa Nabii Muusaa (AS) kwa kificho kikubwa, baada ya Firauni kuteketeza na kuzichinja zayidi ya roho sabiini elfu za Kibani Israaiil.

__________________________________________

*Hili jina la ni jina la cheo aw la mtawala wa Misri , si jina la mtu maalum ; ni sawa na kusema Sultan,Mfalme aw   Raisi.

Bibi Yukabid; mke wa Imraan Yahudi ; Mame Muusaa. hapa baada ya kuzaa hakuwa kama wazazi wengine. Kimaada wazazi huwa na furaha kuu kuwona matunda ya taabu yake ya si chini ya miezi tisa. Mama Muusaa hakuwa hivyo ila alikuwa yeye akichunga kila sehemu ya kiwiliwili chake kwa wingi wa hofu alizokuwa nazo. Kuna wakati hata mtu kayini namna gani, seuze mwenye huruma na hasa awe mwanamke, humjiya huruma aw tuseme ubinadamu. Hayo ndiyo yaliyomjiya mkunga kuwona ule uso wa mtoto mchanga unaong`ara kama usiku wa LAILATU LQADIR . Huruma zake zilimpeleka kwenda kinyume na ile dhamana aliyopewa na Firauni nayo ni ya kupeleka habari ya kila mtoto wa Kibani Israaiil azaliwaye. Si kimbaumbi cha chumba na ukumbi hicho kilichokuwepo ndani ya moyo wa mkunga baina ya kuficha siri hii na kuitowa. Kila akumbukapo makali ya kisu juu ya shingo ya kijichanga hichi pale pale humjiya sura yake yeye mwenyewe - kama hakupeleka habari - kumfika haya, huzidi kufinyangika. Mwisho alipiga moyo konde na kunena:- "Litakalokuwa na liwe. Siri hii siitowi".

Hakuwahi mkunga kukiwuka kizingiti ila yale majasusi ya Firauni yalimuwona. Hapo hapo wakayihujumu nyumba ili wakamnyakuwe huyo aliyezaliwa kama yeye ni mtoto wa kiyume. Nusra wampate huyo mtoto, lakini kuwa qudra na bahati nzuri dada mtu ndiye aliyewawona hawo walinzi katika ufa wa mlango. Hakukasiri ila alijusurisha na kumnong`oneza mama yake, mwili ulichunga sauti yake ilikuwa kama ile ya sahani ya santuri yenye sindano mbovu. Alimnong`oneza mama, " Mama ! askari waja. Wanfika hapo nla................." Mama Muusaa hakungoja kusikiya mwisho wa maneno ila aliruka kuliko ndege na kumbakuwa Muusaa (AS) akamfunika funika kwa matambara na akamtupa tanurini, bila ya yeye mwenyewe kujuwa anafanya nini na kwa nini. Bahati nzuri humo tanurini hamukuwa na moto. Hakuwahi hata kujitenga mbali na tanuri ila askari walikuwa wamejaa nyumba pamoja na kuyipekuwa kila pembe kwa makini na uangalifu mkuu. Hawakuwona mtu ila mama Muusaa kasimama thabiti, shuwari kombe kueleya na ubavuni mwake yupo huyo mwanawe wa kike, kikiri kakara na kazi zake akizifanya kwa upole kabisa, bila ya kuwonesha kuwa ndani ya nyumba kuna kitu aw liko jambo lililotokeya.Askari waliipinduwa nyumba juu chini na walisasambura sawa sawa.

Baada ya wawo kuwona kuwa hawawezi kuwona kitu walimtikisa mame Muusaa sawa sawa na kumtaka awaelezee ukweli na bila ya kificho kitu kilichomleta yule mkunga humu ; akisema uongo ataona cha mtema kuni pamoja na kilichomtowa kanga manyoya.

Yeye aliwajibu moyo imara kuwa huyo mzalishaji ni miongoni mwa wale waliosafiyana niya. Jambo liliomleta hapa ni moja tu, nalo ni wazi kuwa hakujiya jambo lolote ila ni kuzungumza tu. Askari waliondoka hapo mabega yamewashuka kwa kutopata ule mradi wawo.

Yukubid; mama Muusaa alikwisha zake na wenzake kumtafuta Muusaa (AS) lakini ng`o hakumuwona. Baada ya kuemewa na kukata tamaa ndipo aliposikia sauti ya kitoto kichanga upande wa tanuri akamuwokowa mwanawe. Ilikuwa wazi kama muangaza wa mchana kuwa kumficha mtoto ni jambo la muhali. Inawezekana kufanyika hivyo kwa muda tu. Hapo mame Muusaa (AS) aliinama na kuvuta fikira zake zote. Baada ya kupita miezi mitatu. Ilham (Ufunuzi) ya Mola ikamjiya kuwa amtiye mtoto ndani ya kikakasi nacho akitupe baharini. Bahari kwa upande wake itamtupa hapa ufukweni. Hapo atachukuliwa na adui wake na Wangu. Aw kama vile inavyoelezewa  katika Quran Tukufu katika aya hii ijayo:-

Ãóäú ÇÞúÐöÝöíåö Ýöí ÇáÊøóÇÈõæÊö ÝóÇÞúÐöÝöíåö Ýöí Çáúíóãøö ÝóáúíõáúÞöåö Çáúíóãøõ ÈöÇáÓøóÇÍöáö íóÃúÎõÐúåõ ÚóÏõæøñ áöí æóÚóÏõæøñ áóåõ  .

An  qdhiifihi fil Ttaabuuti ; Faqdhiifihi Fii Yammi. Fal yulqihi l Yammu bis Saahili Yaakhudhuhu  `Aduwwun lii wa Lahu (Surat `Taaha : 39).

Mama mtu hakuwa na njiya nyengine ila kufuwata ule wahy wa mbinguni na kufanya vile alivyoamrishwa na Muadiwa. Kikakasi kilijazwa pamba pande zote kabla kutiwa kipenzi Muusaa (AS). Alikuwa mguu nenda, mguu rudi akiyenda zake pwani kulitupa sanduku. Baada ya kulitosa kasha  baharini aliduwaa na kukaa hapo hapo pwani miguu hayiwezi kwenda akiyatazama mawimbi ya maji yakipiga huku na huko, yakenda na kurudi. Alihisi kuwa duniya yote ni hivi hivi na moyo wake bila ya shaka unapiga kuliko hivi. Hakuondoka hapo ufukweni ila baada ya kukamata mkono na mwanawe wa kike na kumongoza mpaka nyumbani.

Pwani walikuwepo watumishi wa kike wa Firauni. Kukiyono tu kikasi walikivamiya na kukinyakuwa na kwenda nacho kama BIARUSI hadi kwa bibi yawo Asiya, mke wa Firauni.

Kitoto kichanga baada ya kufunguliwa kikakasi kilikuwa kimenyanyua uso wake mchesi wenye wingi wa bashasha na unaong`aa na kumtazama Asiya. Moyo wa Asiya ulipasuka "ppaa" na kujaa furaha kwa vile yeye hana mtoto na hii hapa qudra Illahiya  imemleteya mtoto huyu mzuri asiye kifani kuwa ni mwanawe. Akiwa akifikiriya hivi walimjiya askari kumtaka huyo mtoto wakamchinje. Asiya akawambiya wakamwite bwana wawo. Kuja Firauni Bibi Asiya akamuwomba asimuuwe mtoto huyu kwani yeye ni raha ya macho yangu na yako. Usimuue, huenda akatufaa, aw tukamfanya mtoto wetu.

 æóÞóÇáóÊú ÇãúÑóÃóÉõ ÝöÑúÚóæúäó ÞõÑøóÉõ Úóíúäò áöí æóáóßó áóÇ ÊóÞúÊõáõæåõ ÚóÓóì Ãóäú íóäÝóÚóäóÇ Ãóæú äóÊøóÎöÐóåõ æóáóÏðÇ æóåõãú áóÇ íóÔúÚõÑõæäó (9)

Qurratu `Ainin Lil Wa Laka, Laa Taqtuluuhu `Asaa an Yanfaanaa aw Nattakhidhuhuu Walada (Suratil Qasas: 9).

Firauni alikunja uso kama kipande cha papa na kujibu kwa hamaki kuu, "Huyu mtoto mzuri kwako wewe. Mimi sina haja naye katu " Pale pale aliruka na kumyakuwa huku akisema, "Laa ! Sivyo ! Haiwi ! Muhali !  Mtoto huyu hana haki ya kuwishi dakika moja zayidi. Huyu asije kuwa ni katika Bani Israaiil. Haiyumkiniki! Ila hilo. Kumchinja tu. "Palikuwa pata shika, nguwo chanika, chumba kikiruka vumbi na hali halikuwepo kwa wingi wa kufagiliwa. Aibu mwanamke kushindwa katika lile alitakalo na hali yakuwa kapewa kila silaha kali ya kupigana kuliko hizo Tommy gun na stun gun . Asiya alishinda na Firauni akatoka yumo katika kunguruma na kulaani tu. Hapo tena Asiya alipata kazi ya kutafuta mtu wakumyonyesha mtoto. Kwani ilikuwa kila ziwa apewalo yeye halilitaki. Kwa vile alivyokuwa mama Muusaa (AS) kamtowa mwanawe wa kike kutafuta habari zake, kwa kumfuata kwa mbali alitokeya na yeye kufika hapa. Hapo alinena, "Jee, nikuelezeni mtu wa kumtazama na kumshughulikiya kwa kumuoneya huruma na kumnasihi..?" Watu waliokuwepo hapo walinena, "Wewe, bila ya shaka unawajuwa wazee wake. Kwa nini basi ukasema kama hivi. Haya hayasemi ila yule awajuwaye watu wake mtu vilivyo.

Dada yake Muusaa (AS) kwa bahati akaweza kujirusha mbali na mtego huwo, kwa kunena , "Jambo ni wazi na jepesi kuliko hivyo mnavyolifikiri ninyi. Hapana kitu zayidi ila kuwa nawajuwa kuwa wawo ni watu wazuri na wenye tabiya njema na wana huruma sana. Sifa hizi na nyenginezo, zinamvutiya mtoto kuwapenda. Kupewa mwanawe kumjaribu kumyonyesha watu wote hapo walipigwa na mshangawo kwa kumuwona Nabiya Allah Muusaa (AS) alivyolivamiya ziwa na kulinyonya, na hali yakuwa kabla ya hapo kila ziwa alilopewa hakulikubali.

Baada ya kuwonekana kuwa keshapatikana myonyeshaji wa mtoto, walimchukuwa mpaka kwa Asiya * mke wa Firauni kumnyonyesha huyo mtoto mzuri. Asiya alimwambiya mame Muusaa (AS) :- "Unaonaje, si bora ukaye hapa petu ili umyonyeshe huyu mtoto mzuri hapa kuliko kumchukuwa nyumbani kwako ..? Mame Muusaa (AS) akajibu :- " Kama itakupendeza bibiye na kama utanipa ruhusa, basi mimi naoneleya ni bora nimchukuwe kwangu nyumbani. Naogopa watoto wangu wasije kuharibika kama mimi nitakuwa mbali nao. MLEZI WA MTOTO NI MWANAMKE, USISIKIYE YA KUAMBIWA NA WATU WASIYOYAFAHAMU MAMBO VIZURI..".

Baada ya mashindano marefu na pata shika kubwa, mame Muusaa (AS) alipewa ruhusa ya kumchukuwa Muusaa (AS) nyumbani kwake na kumleya pamoja na kumnyonyesha huko huko. Jambo hili la kukaa pahala penye neema na kila raha na starehe na kutaka kwenda kwake na kuhiyari kula ugali na chachu kuliko yale mabiriani na mabaqlawa, huwenda likawastaabisha watu wengi. Wawo kama kidogo tu watazingatiya watajuwa kuwa ule msimamo wake wa inadi ni wa maana kubwa na piya mshangao wawo wote utaondoka pindi sisi tukikumbuka kuwa wanyonyeshaji wote walishindwa kumnyonyesha Nabiyya Allahhi Muusaa (AS) isipokuwa ziwa hili la mama yake mzazi tu ndilo alilolikubali. Kwa hiyo ilimfanya mame Muusaa (AS) awone na kuhisi kuwa yeye ndiye mwenye nguvu hapa sasa kwa vile ajuavyo namna gani Asiya anakipenda hichi kitoto kichanga, Muusaa (AS). Hali ni kama hivyo, kwa nini basi hashiki kani ya kutaka kumchukuwa Muusaa ili huko apate kumuwonesha mapenzi ya dhati ya Umama bila ya kuogopa kitu kwa vile hapana wa kumpeleleza. Huko nyumbani yeye atakuwa mbali na macho ya majasusi wa Firauni.

_____________________________________

*Asiya, mke wa Firauni, inasemekana kwamba alikuwa Muislamu na ndiye aliemuomba Mola wake amjengee nyumba Peponi na amuepushe na Firauni na amali zake mbaya  

Uzuri wake ni kuwa yeye huku atakuwa na uhuru kamili na hata wa kuyamimina mapenzi yake yote yaliyomo kifuwani mwake kwa mwanawe.

Law kwamba yeye kasaliya kwa Firauni, basi moja kati ya mawili lazima ingelimbidi kufanya, nayo yote ni magumu hayatendeki :- Hapo ingelimlazimu kuyaficha mapenzi yake kwa mwanawe aw ingalimpasa ayazike hasa ili watu wasimtiliye shaka baina yake na Muusaa (AS). Nani, jamani, awezaye duniyani kuyaficha kikweli kweli mapenzi yake kwa muda mrefu bila ya kujulikana na mtu ? Taabu ! Vipi tutamtarajiya mama kuyaficha mapenzi yake juu ya mwanawe ? Muhali !

Ilivyokuwa si jambo jepesi mtu kuficha mapenzi yake juu ya mtu fulani kwa watu ;kwa hivyo inaonesha lazima ayaweke wazi, aw laa si hivyo, hawo watu anaowaficha watayagunduwa, kiyama chake ! Mapenzi yake yakiwa yanajulikana, watu watatiya shaka shaka kuwa huyu ni mwanawe. Wakiwa na shaka watamchunguwa na watajuwa. Wakijuwa mauti  tayari.

Copyright ©2004  Uislam.net