BIBI AAMINA

 MAMA YAKE NABII MU`HAMMAD (S. A. W. )

 

Hatutatumiya sana ushahidi wa Quran katika haya yetu mazungumzo. Si kama hakuna, bali tunaoneleya kama itatubidi kuleta ushahidi wo wote kwa ajili ya kutiliya nguvu maneno yetu ; basi tutatumiya Hadithi  zake wetu Mtume (`Alayihi Azkaa Ttahiyya) pamoja na yale waliyoyasema watu juu yake. Mtume (SAW) alikuwa akijisifu kwa kusema maneno yenye maana  ifuatayo :-

لم يزل الله ينقلني من الاصلاب الطيبين الى الارحام الطاهرين , مصفى مهذبا" . لاتتشعب شعبتان الا كنت فى أخيرهما.

 "Lam yazali Llaahu yungiluni mi`na laslaabi ttayyibiina ila larhaami ttaahirati Muusaaffan muhadhdhaban. Laa tatasha`abu shu`ubataani illa kuntu fii akhairihimaa"

{"Mola wangu hakuacha kuniyondosha kuumeni kuzuri na kunipeleka kuukeni safi, tahir na mwenye malezi mema. Kila kukiendeleya kutengana huku kuwili mimi huwa ule upande mzuri zayidi"}

Kwa nini asijisifu namna hiyo aw zayidi na kujinata na hali yakuwa aliyoyasema yote ni kweli, yeye ni mtukufu kwa baba na mama. Hana dowa katu. Mama yake Mu`hammad (Salaawatu Llaahi wa Salamuhu Alaihi) ni Aminah bint Wahab bn Abdul Manaf bn Zuhra bn Kilab bn Murrah. Wazee wake ni mabwana wa Kikureshi, wenye kuidhibiti Makka kwa kila njiya. Na mama yake (wifi yake) ni Birra bint Abdul Iza bn Uthman bn Abdul Daar bn Qusai. Mradi kila mmoja ni miongoni mwa vigogo vya Makka.

Bibi Aamina kakuliya mastakimu mazuri na kulelewa malezi mema. Hakuwa akiyonekana na watu na kucheza ovyo ovyo.  Hapakuwa aliyeweza kuyeleza vizuri sura yake aw umbo lake aw wasfu wake abadan. Mtu hawonekani.

Uzuri wa ubora wake ingawa hawakuwa wakimuwona lakini uliwavutia sana vijana wa Kiqureshi kwa zile habari na sifa zake walizokuwa wakizisikiya. Kila mmoja kati yawo alitamani nyota hiyo iliwachunga yeye. Nyota iliwachagua bwana Abdullah bn Abdul Muttalib bn Hashim  kujuwana na mtoto wa ami yake Aamina bint Wahab, kwa vile ilivyokuwa Banii Hashim na Bani Zuhra ni ndugu na wamoja na hawakutengana tokeya huwo wakati wa babu yake Kilab bn Murrah, nao ni Qusai na Zuhra.

Wote wawili Abdullah na Aamina walikuwa ni wacheza wamoja, walikuwa haweshi kukutana katika michezo yawo ya majumbani. Ilifikiya wakati ikawa lazima Aamina ajifiche ndani na asiyonekane tena na watu, hata na wachezaji wenziwe aw hata na nduguye Abdullah na wenginewo.

Baadhi ya wazee wake Aamina hawakupendezewa sana na ndowa za Abdullah kwa vile wajuavyo habari ya nadhiri ya Abdul Muttalib wakati alipokuwa yeye anachimba kisima cha Zamazam  aw tuseme alipokuwa akikifukuwa, kwani hichi kisima tulieleza nyuma juu ya habari ya Haajir na Nabii Ismaaiil (AS), namna ilivyokuwa hata kikapatikana.

Maqureshi wote walikula njama na kumzuiya Abdul Muttalib asikifikuwe na kumkejeli kuwa yeye ni maskini wa watoto. Hapo aliweka nadhiri kuwa akiruzukiwa watoto kumi na wakawa wakubwa, basi yeye atamchinja mmoja kuwa yeye ni nadhiri yake.

Mambo haya jamani ! Umati wa wake kwa waume wamejazana mbele ya Ka`aba mikono yawo vifuani wanangojeya matokeyo ya kura ya watoto wa Abdul Muttalib. Habari zilitapakaa kuwa kura imemuangukiya Abdullah, na Aamina yupo mtaani. Alizidi kujipweteka kwa habari hii.

Maqureshi wote walimpinga Abdul Muttalib na kumpa shauri ya kwenda kutazamiya huko Khaibar.

Wakatoka pamoja naye. Mji wote haukusaliya mwanamume ila walikwenda pamoja naye. Kwa haya basi, hilaki za Bi Aamina zilizidi kwa kuwona mpaka jiyoni hapana hata mtu mmoja wa kiyume aliyerudi kumpa zayidi ya habari kuwa Abdulla kesha chinjwa aw vipi.

Baada ya siku ishirini msafara wa Maqureshi ulirejeya Makka na shauri ya kupigwa kura kwa kutia mgamiya kumi upande mmoja na wa pili Abdulla. Kama kura ni yake basi wawe wakiyongeza ngamiya kumi kumi hadi Mungu wawo aridhike na kukubali. Haikuchukuwa muda ila Aamina alikuwa machozi yakimtoka kwa furaha ya kuwokoka Abdulla na kutolewa muhanga kwa ngamiya miya moja.

Birra, kwa hakika hakujiya haya, ila alikuwa na matayarisho ya jambo muhimu zayidi. Nalo ni kwa Abdul Muttalib kaja kutaka mkono wa Aamina.

Mashoga na viroro walijaa nyumbani kumpa mkono wa furaha Aamina na kumtoleya kila aina ya hadithi. Hadithi zote zilikuwa ni za wivu na za kumuoneya maya Aamina kwa mchumba wake kichinchiri. Kila mwana kinda kindaki mwana halali wa nyuki alikuwa ananung`unika kwa nini hakuja kuposwa yeye. Usiku ule ule aliyohamishwa biarusi kwake aliyota ndoto ya ajabu. Asubuhi hakuweza ila yeye alimuhadithiya mumewe. Kwa ufupi ndoto ilikuwa :- "KAWONA NURU IKITOKANA NAYE MWILINI MWAKE NA KUNG`ARISHA KILA KITU KILIYOPO KARIBU NAYE, KAMA KWAMBA DUNIYA NZIMA IMEZAGAA NURU HIYO NA HUKU SAUTI ITOKAYO MBALI IKIMWAMBIYA :-

  "WEWE UNA MIMBA YA BWANA WA UMMA HUU."

Baada ya siku kumi hivi Abdulla ilimbidi amuwache Biyarusi kabla ya ule utamu wa fungate hawujesha ili aunge msafara wa biashara unaokwenda Sham - (Syria).

Upepo ulisita na palikuwa kama pana wingu wakati ule Abdulla akimuaga mkewe Aamina. Aamina kila atazamapo kipaji cha Abdulla hawoni ile nuru aliokuwa akiiyona na roho yake nzito kuliko jabali kumuachiliya mumewe kuondoka. Abdulla alijichekesha na kunena : " Ewe mpenzi, si uzuri kuwa mwingi wa huzuni. Baada ya majuma machache tu nitarudi. Jipumbaze na kuvuli changu ambacho kila wakati kitakuwa kikikutembelea..

Bibi Aamina alisaliya kama gogo kasimama penye kizingiti cha chumbani baada ya kuondoka Abdulla. Mpaka akaja Barke mtumishi wake, na kumkamata mkono mpaka kitandani kwake ambapo alikaa siku nenda siku rudi, bila ya kuondoka.

Wakati wa kurejea masafara umekuwa karibu kama pua na mdomo na zayidi kidogo. Bi Aamina yumo kumgoja Abdulla kwa hamu kubwa sana.

Vup ! Aamina anamuwona baba yake, bwana Wahab na mkwewe bwana Abdul Muttalib, mumewe Abdulla hayumo.

Habari za mwisho na za huzuni ndizo zimgojazo : Abdulla yupo Yathrib (Madina) yu mgonjwa, hakuweza kuvumiliya shida za safari. Bora yeye akaye kumuombeya du`aa. Aamina aliendeleya na du`aa kwa muda wa miezi miwili, na huku ndoto nzuri nzuri ya kizazi chema haziishi kumjiya. Yakawa yaliyokuwa. Al Haarith anarudi peke yake kutoka Yathrib na kachukuwa na kubeba mzigo mzito wa huzuni na majonzi :- Abdulla KAFA.

Abdulla kafa ! Hatarejeya ! Aamina aliyona kama kiwingu cha huzuni kimemshukia na duniya yote ilikuwa giza na totoro, imechujuka na wala haina utamu tena baada ya kifo chake Abdulla. Ajabu hii hata machozi yanafanya ubakhili na hayataki kuchiririka ? Kwa nini isiwe hivyo na hali yakuwa maiti ni kijana mbichi wa miaka kumi na nane..?!

Majonzi na fikira za faida gani kutolewa ule muhanga wa  ngamiya miya moja, na hali ya kuwa huyo aliyetolewa muhanga huwo ilibidi afe. Majonzi yaliondoka mara tu baada ya kujuwa muhanga ule ulikuwa ni kwa sababu ya hicho kizazi kitukufu kiliyomo tumboni mwake Aamina. Mwezi wa Mfungo sita aw Agosti 570 Nuru Tukufu iliyanza kuzagaa na kutanda mote kwa miyezi michache baada ya kifo cha baba yake, Abdulla.

Ukisoma habari za maisha ya Nabii Mu`hammad (SAW) utawona fikra zinagongana. Kuna wasemawo kuwa baba yake kafa kabla ya kuzaliwa kwake. Wengine wanasema kafa baada ya kuzaliwa. Piya hawa wanatofautiyana huko kufa kwake kwa muda gani, tokeya majuma mawili  tangu kuzaliwa kwa mtoto hata kwa  wa miyezi kumi na moja.

Yenye nguvu zayidi ni kufa kabla ya kuzaliwa. Ilichukuwa kiasi cha siku khamsini tokeya kushindwa Abraha kuipiga L-Ka`aba  na kuzaliwa kwa Mu`hammad (SAW). Wengine wanasema siku ile ile na wengine wanasema mwaka ule ule.

 Usiku wa manane ndoto nzuri zilimjiya Aamina. Sauti nzuri ilimwambia :-

                   أعيذه بالواحده من كل حاسد , وسميه محمد.

Aidhiihi bil waahid, min kulli haasidi, wa Sammiihi Mu`hammadi.

{"Mkinge kwa Wahedi, na shari za hasidi, umwite Mu`hammad}

Baada ya ndoto hii aliyota nyengine kuwa kazungukwa na wanawake wengi pande zote za kitanda. Hakuwafahamu kina nani ila aliyona kuwa wawo ni kama Maryam bint `Amraan, na Asiya mke wa Firauni, na Haajir mame Ismaaiili. Papo hapo akazaa NURU TUKUFU  na miujiza namna kwa namna ilitokeya.

Kwa kishindo cha kifo cha mumewe, maziwa ya Aamina yalikawuka na asiweze kumnyonyesha mwanawe. Kwa hivyo akapewa Thuwayiba, ambaye aliwahi kumnyonyesha ami yake Hamza bn Abdul Muttalib mpaka waje mamama walezi aw kwa jina jengine wanyonyeshaji. Ambawo karibu wote baada ya kufika walimkataa kwa vile yeye ni masikini na ni yatima. Aamina yalimjaa majonzi kuyawona haya.

Huzuni hizi ziliondoka jioni baada ya kuondoka Halima Ssa`adiya, ambaye karejea kumchukuwa kwa vile wenziwe walirejeya na watoto ila yeye ; kwa hivyo aliona haya kurejeya mikono mitupu. Bora kupata japo nusu ya ole kuliko kuondokeya patupu.

Halima kumchukuwa Mu`hammad (SAW) miyujiza iliyanza. Chuchu zilijaa maziwa, na hata ngamiya wawo alijaa maziwa. Neema ya maziwa ya wale wanyama wake iliendeleya.

Nyumba ilikuwa nzito na ilimuinamiya Aamina kwa vile mumuwe kafa na alisaliya na maliwazo mamoja tu nayo  ni kiliomo tumboni mwake. Lewo kitu hicho kipo duniyani nacho hakipo hapo nyumbani, bali kipo huko katika jangwa la Bani Saad. Hapana kitu cha kumpumbaza ila majonzi na huzuni ambazo zilimuathiri sana afiya yake.

Hayikuchukuwa muda ila miyaka miwili ilikwisha kama mchezo na Halima alirejeya na Mu`hammad (SAW) anataka kutumbuka kwa wingi wa damu iliokuwa ikimwenda mwilini. Halima alimpembejeya sana Aamina amuwachiliye yeye huyu mtoto amlee, kwa vile mjini jangwani kuna hewa safi na upepo mzuri mpaka akapewa.

Halima kwa ghafla tunamuwona yu njiyani kambeba Mu`hammad (ASS) akirudi naye kwa Aamina kwa hofu ya wale Malaika wawili waliompasuwa tumbo na wale makohani waliyotaka kumchukuwa. Waandishi wengine wa tarehe wanasema Mu`hammad (AS) alikaa kwa Bani Sa`ad hadi kufika hirimu kidogo ndipo walipomrejesha.

Kutimu Mu`hammad (ATT) miyaka sita Aamina alifunga safari yeye na mwanawe kwenda Yathrib kulizuru KABURI TUKUFU. Nyumba yake aliitazama kwa jicho la muagano, na baada akenda Ka`aba kuzunguka kwa kuiaga.

Aamina njiyani alimlowanisha Mu`hammad kwa vile kumbusu na kumkumbatiya mpaka wakafika huko salama. Kiyasi cha mwezi Aamina hakuwa na kazi ila kwenda maziyarani na kujipumbaza na kusema na kaburi na kuliliya hadi macho yakachoka huko kuliya. Wakiwa njiyani katika msafara wawo wa kurudi Makka ulivuma upepo mkali sana, hata ikabidi wasite na kule kuendeleya na safari. Hapa nguvu za Aamina ziliyanza kidogo kidogo kutoka.

Alinusurika na kumkumbatiya Mu`hammad (SAW) huku yumo kunena maneno yake ya mwisho :-

 "Kila chenya uhayi na kufa ni lazima, kipya huchakaa. KIKUBWA CHO CHOTE HUTOWEKA. MIMI NAFA NA MAKUMBUSHO YAPO. NIMEYACHA KHERI NA NIMEZAA KITU SAFI NA TAHIRI ".

Duniya yote imejiinamiya, kila kitu kimejaa huzuni hapana sauti kusikilizana aw kitu cho chote kutaharuki. Mu`hammad (SAW) kayinama juu ya kiwili wili cha maiti ya mama yake. Mu`hammad (SAW) hujisifu na kunena :- Mimi ni mwana wa mwanamke wa Kikureshi alaye nyama ya kukausha kama ng`onda" Na mimi ni mtoto wa kina Aatika katika Bani Saliim.

 

Copyright ©2004  Uislam.net