MASUALA MUHIMU YA  KUJIULIZA

  1.  Je UKIMWI ni adhabu itokayo kwa Allah na kwa hivyo hakuna haja ya kutafuta kinga au tiba au ni maradhi kama mengine inabidi kinga na tiba zitafutwe?

Kwa mtazamo wa Kiislamu maradhi yoyote ni mtihani kwa waja kutoka kwa Mungu ili awatizame watafanya nini katika mtihani huo hivyo unaweza kuwa adabu au  njia ya kupandishwa cheo . Lakini jambo ikiwa ni mtihani au ni adhabu kutoka kwa Mungu haina maana kwamba halifai kulitafutia tiba au kinga.

Kwa hivyo ni lazima kutafuta kinga na tiba ya UKIMWI na ya maradhi mengine ijapokuwa maradhi hayo ni adhabu au la.

   2. Je mtu aliyepatwa na maradhi ya UKIMWI anakuwa amelaaniwa na ni muovu au mbali na mambo hayo?

        Aliyepatwa na UKIMWI hawezi kushutumiwa kuwa amelaaniwa au ni mwovu mpaka ithibiti kuwa ni muovu katika matendo yake au kauli zake kama ilivyo kwa wagonjwa wanaopatwa na maradhi ya aina nyengine. Kwani UKIMWI waweza kuambukizwa pia kwa sababu nyengine ambazo si za haramu  wala si za makosa yanayowajibisha laana za Mungu. Njia hizo ni kama maambukizo kutoka kwa mume au mke wa halali , au kwa njia ya kutiwa damu au kunyonya n.k.

3.  Ni wajibu upi wa kidini unaomwajibikia aliyepatwa na UKIMWI?

      Aridhie kuwa hiyo ni Qadar yake kutoka kwa Mungu, astaghafiru sana kwa Mungu, asizidiwe na mawazo na masikitiko na wala asieneze maradhi haya kwa wengine. Bali afuate vilivyo maagizo ya wataalamu na ya washauri nasaha.

4.  Ni wajibu gani wa familia kwa mgonjwa wa UKIMWI?

Wawe wapole kwa muathirika wala wasimtenge kwani UKIMWI hauenei kwa kukaa na mgonjwa, kula nae au kwa kubadilishiana nguo. Hata hivyo ni vyema wawe waangalifu katika matumizi ya vyombo na zana zilizoingia damu.

5.  Ni wajibu gani kwa jamii kwa wenye UKIMWI?

Wamhudumie vyema mgonjwa, wamjali, wasimtegenge na wasimnyanyapae au kumuaibisha. Hayo ndiyo mafundisho ya Mtume S.A.W. alipokuwa akielezea namna ya kuishi na mgonjwa aliposema: (Wahurumieni waliopo ardhini, na  yeye aliyeko juu atakuhurumieni). Akasema tena S.A.W. katika hadithi nyengine (unapokwenda kumzuru mgonjwa,  basi zungumza maneno mazuri matupu...)

Hata hivyo  pia inabidi pachukuliwe hadhari ili pasije pakatokea maambukizo mapya kwa wengine.

Copyright ©2004-2005  www.uislam.net