|
UKIMWI (AIDS) husababishwa na nini?
UKIMWI husabaishwa na viini vidogo sana kupita kiasi vyenye uhai ambavyo
wataalam huviita "VIRUS" au KIRUSI. Hivi ni viumbe vidogo sana sana
ambavyo havionekani kwa macho wala kwa darubini za kawaida. Viumbe wa
kabila hili la "virus" wapo wa aina nyingi na hutofautiana kwa maumbile
na kwa madhara au magonjwa wanayoleta. Kwa mfano kuna virus wanaoleta
ugonjwa wa mafua; na kuna virus wanaoleta ugonjwa wa surua; n.k.
Kwa kawaida mwili unao katika damu chembechembe maalum ambazo hutumika
kama askari au silaha za kupigana na maadui, yaani viini vinavyoleta
magonjwa. Viini vinavyoleta UKIMWI (AIDS) vikipata nafasi ya kupenya na
kuingia katika damu yako vitaanza kuingia ndani ya baadhi ya
chembechembe hizo maalum ambazo ndizo zenye jukumu la ulinzi na usalama
mwilini. Baadhi ya chembechembe hizo zilizoingiliwa huweza kufa baada ya
muda wa siku 20 hivi; baadhi nyingine huenda zikadhurika lakini zisife;
na baadhi nyingine huenda zikadhurika kidogo tu. Kwa vyovyote viini vya
UKIMWI ni kiboko kikali kwa chembechembe hizi ambazo ni baadhi ya silaha
muhimu za mwili.
Viini vya UKIMWI vitakavyoingia ndani ya chembechembe hizo maalum za
kujihami vitaweza kuendelea kuzaana humo na baadhi yake vitaweza hata
kutoka na kuingia katika ubongo ambako vitaweza kujificha ama kuendelea
kuzaana.
Viini hivyo vya UKIMWI vinapoendelea kuishi mwilini mwako huenda mambo
matatu yakaweza kutokea baada ya kupita muda wa miezi minne mpaka miaka
mitano au zaidi.
1.
Utaweza kunyemelewa na magonjwa ya hatari ambayo
yatakuletea kifo. Jambo hilo likitokea tutasema umepatikana na UKIMWI
Moto.
2.
Utaweza kunyemelewa na magonjwa rejareja yasiyoweza kuleta
kifo. Jambo hilo likitokea tutasema umekumbwa na UKIMWI Vuguvugu.
3.
Utaweza kuendelea kuwa na afya nzuri kama kawaida ya watu
wengine. Jambo hilo likitokea tutasema kwamba UKIMWI ulionao ni
Baridi.
a.
UKIMWI Moto:
Endapo viini vya UKIMWI vilivyoko mwilini vitafaulu kwa kiasi kikubwa
kuvuruga silaha zako za kujihami, basi mwili wako utakuwa na uwezo mdogo
wa kupambana na magonjwa. Viini vya (magonjwa maalum mbalimbali ambavyo
hapo awali vilikuwa havithubutu kukuingilia sasa vitakunyemelea kwa vile
wewe umekuwa askari asiye na silaha zake kamili za kujitetea. Kwa mfano
kama viini vya magonjwa ya tumbo, au vya magonjwa ya kifua vitabahatisha
kuingia mwilini mwako kwa njia yoyote ile, vitakuta hakuna upinzani
mkali; na kwa hiyo magonjwa hayo yatapata mteremko wa kukufyeka. Ukweli
ni kwamba ukikumbwa na UKIMWI moto kitakachokuua sio viini vya UKIMWI
moto kitakachokuua sio viini vya UKIMWI bali ni hayo magonjwa mengine
yatakayokunyemelea kutokana na hali yako duni ya kujihami.
b.
UKIMWI Vuguvugu: Endapo silaha zako za kujihami hazitavurugika
sana basi uwezo wako wa kujihami hautakuwa duni sana, na kwa hiyo viini
vya magonjwa vitakavyojaribu kukunyemelea vitakiona cha mtema kuni. Hata
hivyo utakuwa unasumbuliwa sumbuliwa na magonjwa. Lakini wakati mwingine
huenda huo UKIMWI wako uliyo vuguvugu ukaweza kubadilika na kuwa UKIMWI
Moto kufuatana na mabadiliko fulani fulani yatakyoweza kutokea mwilini
mwako, ama katika hivyo viini vya UKIMWI vitakavyoendelea kuishi mwilini
mwako.
c. UKIMWI Baridi:
Endapo viini vya UKIMWI vilivyoingia mwilini vitashindwa kuvuruga silaha
zako za kujihami basi wewe hutasumbuliwa na magonjwa ya kunyemelea ama
kuotea, na afya yako itaendelea kuwa ya kawaida. Isipokuwa yawezekana
pia huo UKIMWI wako baridi ukaweza kubadilika hapo baadaye na kuwa
vuguvugu au moto kutokana na mabadiliko yatakayoweza kukutokea wewe au
kutokea hivyo viini vya UKIMWI vilivyomo mwilini mwako.
|