UJUWE UISLAMU

 

Ø   Uislamu: Dini aliyoiridhia Allah, na maana yake ni “Kujisalimisha Mja kwa Allah kwa kufuata Sharia yake”.

Ø   Allah: Jina la aliyeumba kila kitu -hata sehemu na wakati-, hajafanana na chochote, habadiliki, ni Mkamilifu wa Dhati kwa kila Sifa, hahitaji, hana mwanzo, wala hatuwezi kumfikiri wala kumuona, na yeye haonekani kabisa.

Ø   Muislamu: Yeyote aliyejisalimisha kwa Allah kwa kukubali kufuata Sheria yake. Mtu atakua Muislamu kwa kushuhudia mambo matatu:

1.     Kua hakuna wa kuabudiwa kwa Haki isipokua Allah.

2.     Kua Muhammad ni Mtume wa Allah.

3.     Kua aliyokuja nayo Muhammad ni Haki inayotoka kwa Allah.

Ø   Nguzo za Uislamu: Shahada, Sala, Zaka, Funga, na Hija.

Ø Shahada: Neno la Ahadi ya kuingia katika Dini ya Uislamu nalo ni: Ninashuhudia kua hakuna wa kuabudiwa kwa Haki isipokua Allah, na ninashudia kua Muhammad ni Mtume wa Allah, na nimekubali kua aliyokuja nayo Muhammad ni Haki inayotoka kwa Allah.

Ø   Sala: Ibada maalumu inayolazimika kila siku mara tano, iliyokusanya Takbira, Kusoma Qurani, Kurukuu, Kusujudu, Tasbihi na, Salamu.

Ø  Zaka: Fungu maalumu linatolewa na Matajiri katika Mali zao, kila mwaka mara moja kwa ajili ya Mafakiri, Masikini, Kuunganisha Nyoyo, Wenye kuikusanya, Wapita njia, Waliozidiwa na Madeni, Ukombozi wa Watumwa na Njia ya Allah.

Ø   Funga: Kujizuia na kula, kunywa, kuingiliana kindoa, na kila kosa kubwa kuanzia kuchomoza kwa Alfajiri mpaka kuzama kwa jua wakati wa Magharibi kwa nia ya Ibada, kwa mwezi mzima wa Ramadhani, nao ni mwezi wa Tisa kwa mujibu wa Kalenda ya Kiislamu.

Ø  Hija: Ibada maalumu ya Kuitembelea Al-kaaba, na sehemu takatifu zilizoko Hijaz katika Mji wa Makka katika mwezi maalumu wa Hija.

Ø    Sheria: Mafunzo ya Mtume katika Mitume ya Allah.

Ø Mtume: Mtu aliyepewa Sheria kutoka kwa Allah, muda wake utamalizika kwa kuja Mtume mwengine baada yake, na kila watu wanalazimika kufuata Sheria ya Mtume wao.

Ø  Muhammad: Mtume wa mwisho katika Mitume ya Allah. Na yeye amefuta Sheria za waliopita kabla yake: Nuuh, Ibrahim, Mussa, Daudi, Sulaiman, Issa mwana wa Maryam, n.w. wala hakuna Mtume mwengine baada yake.

Ø   Qur-ani: Kitabu alichopewa Mtume Muhammad, kilichokusanya Sheria ya Allah, nacho ni Dalili ya Utume wake, na hakuna kitabu kilichokua na mfano wake. Allah amechukua ahadi ya kukihifadhi, basi kimehifadhiwa kwa Lugha yake, Muandiko wake, na Visomo vyake kizazi kwa kizazi, nacho ni msingi wa mwanzo wa Sheria katika Uislamu.

Ø Sunna: Yaliyo sahihi katika kupatikana kutoka kwa Mtume (s.a.w) ikiwa ni Maneno, Vitendo au Maridhio kwa yaliyofanywa, nao ni Msingi wa Pili wa Sheria katika Uislamu.

Ø   Ijmaa: Makubaliano ya Wanavyuoni wa Kiislamu katika Hukumu ya Kitu iliofichika Hukumu yake, bila ya kwenda kinyume na yaliyomo katika Qur-ani na Sunna sahihi. Ijmaa ni Msingi wa Tatu katika Misingi ya Sheria katika Uislamu.

Ø  Hukumu: Katika Uislamu kuna Hukumu tano; jambo lolote halitoki nje ya Hukumu hizo tano, nazo zinathibiti kwa hiyo Misingi ya sheria ya Uislamu, nazo ni Wajibu, Haramu, Man-duubu, Mak-ruuhu, na Mubaah.

Ø   Wajibu: Ni Hukumu inayojuilisha kulazimika kukifanya kitu, anayefanya Wajibu anapata Thawabu, anayewacha anapata Kosa la Dhambi kubwa; k.m: Kuwatii Wazee, kusali, kufunga, kuhiji.

Ø   Haramu: Ni Hukumu inayojuilisha kulazimika kukiacha kitu, anaefanya Haramu anapata Kosa la Dhambi kubwa, anaewacha anapata Thawabu; k.m: Kuzini, Kulewa, kuvuta Sigereti.

Ø   Man-duub: Ni Hukumu anayojulisha kupendelewa kitu, anayefanya Man-duub anapata Thawabu, anayewacha hana Kosa; k.m: Kuandikiana wenye kudaiana walio waaminifu.

Ø  Mak-ruuhu: Ni Hukumu anayojulisha kuchukizwa kitu, anayewacha Mak-ruuhu anapata Thawabu, anayefanya hana Kosa; k.m: Kukaa na mwenye kutuhumiwa katika Dini.

Ø   Mubaah: Ni Hukumu inayojuilisha kua kinachokusudiwa hakimo katika moja ya Hukumu yoyote miongoni mwa hizo zilizopita; k.m: Kujichagulia chakula katika yaliyo Halali, na Mja katika Mubaah analipwa kwa mujibu wa Nia yake.

Ø   Nguzo za Imani: Kuamini: Allah, Malaika wake, Vitabu vyake, Mitume yake, Siku ya Mwisho, na Kadari ya Allah katika Matokeo yote.

Ø   Allah: Jina la yule aliyeumba kila kitu, asiyekua na mwanzo wala mwisho, kuwepo kwake ni kwa lazima, yeye ni mkamilifu wa dhati"

Ø Malaika: Viumbe wa Allah wasio muasi, wasioacha Ibada, wenye kufanya kila Amri wanayoamrishwa, hatuwezi kuwaona, wako wanaoandika na kushuhudia yote wanayoyafanya Waja wa Allah, wao wameumbwa kwa Nuru.

Ø   Vitabu: Maandiko maalumu aliyoyajaalia Allah kua ni mkusanyo wa Sheria za Mitume; vikiwemo Zaburi cha Mtume Daudi, Taurati cha Mtume Mussa, Injili cha Mtume Issa na Qur-ani cha Mtume Muhammad. Na vitabu hivyo hakuna kilichobakia katika Asili yake isipokua Qur-ani peke yake.

Ø  Mitume: Watu aliowateuwa Allah kua ndio njia ya kufikisha Sheria zake kwa Waja wake, wao wamehifadhiwa na Makosa makubwa, wanapata Ufunuo utokao kwa Allah, na wao ni Hoja juu ya Waja. Mitume ni wengi sana miongoni mwao ni Nuuh, Huud, Swaleh, Ibrahim, Is-haka, Is-mail, Yaaqub, Yuusuf, Yuunus, Luut, Id-ris, Daud, Sulleiman, Mussa, Yahya, Issa, na wa mwisho wao ni Muhammad (s.a.w), na kila Mtume inamalizika Ahadi yake kwa kuja Mtume wa mbele yake.

Ø   Siku ya mwisho: Siku ya Malipo, ukubwa wake ni sawa na mika 50,000 ya hapa Duniani, watasimama watu wote kwa ajili ya kulipwa kila mmoja kwa Imani yake na matendo yake, aliyekua mwema kwa Kuifuata Sheria ya Mtume wake aliyepelekwa katika zama zake; huyo atalipwa makazi mema katika Pepo yenye kudumu, atapata humo kila analolitamani; na aliyekua Muovu kwa Kumuasi Mtume wake, na yeye hakutubia, huyo atakua katika Adhabu yenye kudumu ya Motoni, kwa mujibu wa Makosa yake, Allah atuepushe nao (Amin).

Ø Kadari: Makadirio ya mambo yote yatakayotokeza katika viumbe tokea kuanza kuumba, nayo ni Siri ya Allah mtukufu, sisi ni juu yetu kujitahidi kwa kufuata Sheria ya Allah, na huku tunaamini kua hakuna linalotokezea isipokua Allah ametaka litokeze ikiwa ni Zuri au Baya, kwa sababu Allah haasiwi kwa kushindwa, wala haadhibu kwa kudhulumu, na yanayowapata Waja ni kwa Mavuno ya Utiifu au Kuasi kwao, au hua ni Mtihani kwa Waja wake.

Ø  Watu ni watatu: Muumini, Mnafiki na Mshirikina, mtu yeyote atakua ni mmoja katika hawa; na yeye atakua ima Muislamu au Mshirikina, na atakua ima Muumini au Mkafiri.

Ø   Muumini: Aliyekubali Sheria ya Allah na Ikamuhukumu katika Maisha yake katika fikra, maneno na matendo yake.

Ø  Mnafiki: Aliyekubali Sheria ya Allah lakini yumo katika Kumuasi Allah kwa kosa kubwa katika fikra, au maneno, au vitendo vyake, mpaka atubie kwa Allah.

Ø   Mshirikina: Anayeabudu asiyekua Allah, au kumshirikisha na chengine katika Ibada, au kumkataa, au kupinga Hukumu iliyomo katika Sheria ya Allah inayojulikana katika Uislamu kwa yakini, na kwa makubaliano.

Ø  Muislamu: Muumini na Mnafiki.

Ø  Mkafiri: Mshirikina na Mnafiki.

Ø  Ukafiri: Kumuasi Allah kwa kosa kubwa lolote, nao umegawika vigao viwili: Ukafiri wa Kinafiki na Ukafiri wa Kishirikina.

Ø   Ukafiri wa Kinafiki: Kumuasi Allah kwa Kosa Kubwa lisilokua la ushirikina, mwenye kua na sifa hiyo atapata haki zote za Waislamu isipokua Walayah.

Ø Walayah: Mapenzi kwa ajili ya kumtii Allah, kwa kusaidia, kupenda, kunusuru, kurehemu, na kuridhia.

Ø  Ukafiri wa Kishirikina: Kumuasi Allah kwa Kosa la ushirikina, mwenye kosa hilo hana haki yoyote ya Kiislamu, na haki yake ni Baraa-a.

Ø   Baraa-a: Kinyume cha Walayah, nayo inalazimika kwa kila mwenye sifa ya Ukafiri, kwa sababu kila Kafiri ni Adui wa Sheria ya Allah, basi laana ya Allah inakua juu yake mpaka atubie.

Ø Mezani siku ya Malipo: Kila mja yatapimwa Matendo yake siku ya Malipo, Ima mezani zake zitakua mzito au zitakua nyepesi.

Ø Mezani mzito: Mezani za Mja zitakua mzito kwa kukubaliwa Mema yake hata kama ni Jema moja, atalipwa kwa hilo Jema lake, na kuongezewa na Allah mtukufu, na yeye atakua katika Makazi mema katika Pepo bila ya Kuadhibiwa katika Moto, na Allah anayakubali ya Waumini Wachamungu.

Ø  Mezani nyepesi: Mezani za Mja zitakua nyepesi kwa kukataliwa Matendo yake, kwa sababu ya Maasi yake makubwa, ikiwa hakutubia kwayo, kwa sababu Allah hasamehe kwa aliyeendelea na Dhambi kubwa mpaka yanapofika Mauti anasema: Ninatubia hivi sasa”, na Allah haridhii watu Mafasiki; basi mtu huyo atakua katika Adhabu ya Motoni kwa Mujibu wa Makosa yake, na yeye humo atabakia Milele bila ya kukoseana au kutoka.

Ø   Shafaa: Uwombezi wa Mtume siku ya Malipo, nao wataupata Waja wema aliowaridhia Allah tu, kwa kukubaliwa Toba zao, na kupandishwa Daraja zao, na kuondolewa kwa Mazito ya Siku hiyo, kutokana na yale Makosa ambayo walitubia kwayo; wala hakuna Shafaa kwa Waovu madhalimu wa nafsi zao, hawakutubia kwa Maasi makubwa waliyoyafanya, kwani Allah haridhii watu Mafasiki.

Ø  Jihadi: Kujitahidi kwa kila njia ya kuiweza Nafsi katika kuyahama Mabaya, na kuichukua kwa mujibu wa Sheria ya Allah, na kuilinda Dini na Njama za Maadui,  na kuindeleza kwa njia za Sheria; kama Kusomesha, kuitangaza, kushikamana nayo katika raha na shida, wepesi na uzito bila ya khofu, wala aibu, wala haya, na kuzuia Uadui dhidi ya Waislamu.

Ø  Hijrah: Kuhama kwa Mtume Muhammad (s.a.w) toka Mji wa Makka kwenda Mji wa Madina, na ndipo ilipoanza Tarekhe ya Uislamu ndani ya Sheria ya Mtume Muhammad kwa Ijimaa ya Maswahaba (r.a).

Ø   Sahaba: Kila aliyekutana na Mtume -katika Uhai wake- hali ya kua ni Muislamu na akafa katika Hali hiyo.

Ø  Shetani: Kila mwenye kumuasi Allah kwa makosa Makubwa na kufanya kila Juhudi za kuwapoteza wengine na kuwaingiza katika Kufuru.

Ø  Ibilisi: Shetani wa mwanzo, ni katika Majini huyo, aliifanyia Kiburi Amri moja tu -ya kumsujudia Adamu-, basi alilaaniwa na kufukuzwa, kwani alikataa kutubia, lakini alichukua Ahadi ya kukipoteza Kizazi cha Adamu.

Ø   Jini: Kiumbe alichokiumba Allah kutokana na Moto, hatuwezi kukiona, na wao wanazaliana, na wanaishi, wako Waislamu kati yao, na wako wasiokua Waislamu.

Ø   Maamrisho: Kumtakasa Allah na Kufanana na Viumbe, au Viumbe kufanana na Allah. Kukubali kua Muhammad ni Mtume wa Allah. Kusimamisha Sala katika Wakati wake. Kutoa Zaka nayo ni 2.5% kila mwaka baada ya kutimiza kiwango cha 85g za Dhahabu au 600g za Fedha, pia kuna Zaka ya Wanyama kwa Wafugaji wa Wanyama wa Miguu minne, na Zaka ya Mazao ya Nafaka za kula kwa wakulima ni 10% kwa asiotilia maji na 05% kwa wanaotilia maji. Kufunga mwezi wa Ramadhani. Kuhiji na Umra kwa mwenye uwezo. Wasia kwa Jamaa wasiorithi. Kuwafanyia wema Wazazi wawili, Jamaa, Jirani, Masikini, Rafiki, Mpita njia na Mgeni. Kutia jando kwa Mwanamme. Kuoga Baada ya Hedhi na Nifasi kwa Mwanamke. Usafi. Kuoga Janaba baada ya kuingiliana au kutokwa na Maji ya Uzazi. Udhu kabla ya Sala. Kukata kucha kila wiki. Kunyoa sehemu za siri kila mwezi. Kuacha ndevu. Kupunguza masharubu. Kuamrisha Mema na kukataza mabaya. Kutaka Idhini ya kuingia katika Nyumba. Kutoa Salamu. Kurejesha Salamu, Heshima kwa wakubwa. Kuwarehemu wadogo. Ukweli katika maneno na ahadi. Uaminifu. Kutafuta Riziki ya Halali. Kuondosha Maudhi. Kutafuta Elimu. Kuhifadhi utupu. kukwepusha Jicho kwa kutoangalia ya Haramu. Kuvaa kwa kuyasitiri aliyoamrisha Allah yasitiriwe -kwa mwanamme kutoka Kitovu mpaka Magoti, kwa mwanamke ni mwili mzima isipokua Uso na Viganja-. Sadaka. Kutubia. Kusamehe. Kusimamisha Ushahidi kwa wakaribu na wambali. Kuoa kwa asiyeweza kujizuia. Kumtunza Yatima na mali yake. Kutembelea mgonjwa. Kumkosha Maiti wa Kiislamu, kumsalia na kumzika. Mirathi kama alivyogawa Allah katika Qur-ani. Kusimamisha Uadilifu kwenye uwezo. Kuwahudimia Wake na watoto. Kuwahifadhi Wazazi na kuwatii, Kumpenda mwenye Kumtii Allah na Mtume wake. Kuwatii viongozi Waumini Waadilifu. Kujifunga na Wanavyuoni Waumini. Hailazimishi Allah Nafsi yeyote nje ya Uwezo wake, na yeye anawapenda wenye kutubia na wenye kujitakasa na makosa na uchafu.

Ø  Makatazo: Kumshirikisha Allah kwa kumfanyia msawa katika Sifa, Ibada na Sheria (Amri na Makatazo). Kuvunja undugu. Kulewa. Kuzini nako ni kumuingilia mwanamke bila ya ndoa. Ndoa ya waliozini, Kulawiti nako ni kuingilia katika Utupu wa nyuma. Kusagana nako ni kupitisha matamanio ya kuingiliana baina ya mwanamke kwa mwanamke. Kuikaribia Zinaa nako ni kuingia katika kila kinachopelekea kuzini k.m: Muziki, kuangalia, kukonyeza, kugusa, kufikiri, kujitoa matamanio kwa kujichezea. Kuiba. Kiapo cha uongo. Kusengenya nako ni kumsema mwenzio kwa asiyoyapenda. Kufitini nako ni kuchukua na kupeleka maneno kwa kusababisha ugomvi na chuki. Uongo. Khiyana. Kujisemea bila ya Elimu. Kuwaudhi Wazazi. Kuasi amri ya kiongozi muadilifu. Kula maiti, nguruwe, damu, najisi, uchafu, punda, kilichochinjwa bila ya kutajwa Allah juu yake, na kila chenye meno ya ncha katika wanyama, na chenye kuwinda kwa makucha katika Ndege. Kujiua. Kuidhuru Nafsi. Rushwa. Khadaa. Shahada ya Uongo. Kudhulumu. Kuua Nafsi bila ya Haki. Kuua watoto. Kumkaripia Masikini. Kuishi na zaidi ya Wake wanne. Kiburi nako ni Kudharau Haki, na kujiona mbele ya watu. Kutembea kwa maringo. Kudanganya katika vipimo. Uhasidi nao ni kutamani kuondoka neema ya mwenzako. Kutembea Uchi. Kuvaa mwili wako hasa kwa mwanamke. Kujifananiza na Jinsi nyengine; mwanamke kujiingiza ya wanaume kitabia, kimavazi, kimaumbile, na mwanamme kujiingiza ya mwanamke katika hayo; kama kuvaa Dhahabu au Hariri. Kujibadilisha kimaumbile k.m kinyoa nyusi, kuunganisha nywele, kuchonga meno, kupaka nyeusi kwa kuficha mvi. Kula Riba nayo ni ongezo kwa mujibu wa wakati katika jinsi ya kitu. Kamari nayo ni pato linalopatikana kwa kukusanya vya wengi kisha akapewa mwenye kuangukiwa na kura na ndio wakaipa jina la Bahati na sibu ((Nipate au nikupate)). Uadui. Kusaidia katika Dhambi na Uadui. Kumpenda mwenye kumuasi Allah na Mtume wake. Na Allah anawapenda wenye kutubia na kujitakasa.

Ø   Neema: Kila alilotupa Allah katika Uhai huu ni Neema kwetu sisi Waja wake, basi ni wajibu wetu sisi Waja  kumshukuru Allah katika Neema zake zote.

Ø  Kushukuru: Kizitumia Neema za Allah katika anayoridhia Allah, Mja atapata Barka na Nyongeza katika Maisha yake iwapo atashukuru;  hata ikiwa ni Baya kwa kusubiri kwani huo ni Mtihani.

Ø   Tahadhari: Watu wengi wamepotea kwa sababu tatu: Kukipa kiumbe Sifa ya Muumba, Kumpa Muumba Sifa ya Kiumbe, na kuitakidi Usamehevu bila ya Toba; na huu wote ni upotevu katika Sifa za Muumba. Allah ametakasika na kila Upungufu na Kuhitaji, na kwenda kinyume na aliyoahidi kwa Mitume yake (s.a.w); atuepushe Allaha na Udhalimu wa kufuata Mapendwa moyo (Amin).

Ø  Kukipa kiumbe sifa ya Muumba: Hawa ni wale waliopotea kwa kujifanyia Mungu katika Vuimbe, ima Watu katika Mitume, Wafalme, na Waja wema, Miti, Milima, Makaburi, Masanamu, n.v. wao wanaviomba na kuviabudu, wanavipa uwezo wa aliyeumba kua navyo vinadhuru na kufaa, vina Amri na Katazo, vinalipa na kuadhibu, ni vya Tangu havina Mwanzo n.m.

Ø   Kumpa Muumba sifa za Viumbe: Hawa ni wale walioitakidi kua Muumba anahitaji vitu vyengine katika Ufalme wake, wakaitakidi kua yeye ana Sehemu, Sura, na Viungo vyote isipokua Uchi na Ndevu, anashuka na kupanda, wako waliosema yeye ni kama sisi, na wengine wakajificha kwa neno lao: Yeye sio kama sisi, lakini hayo anayo kiuhakika, na Uhakika wake anaujua yeye mwenyewe.

Ø Zinduka: Sifa za Allah ni Maana za kuzingatia Ukamilifu wa Allah, na sio kitu chengine kilicho nje ya Uhakika wake, kwa sababu yeye ni Mkwasi hategemei wala hahitaji. Ametakasika na kila sifa inayolazimisha kupatikana chengine ndio nayo ipatikane k.v: Mkono, Mguu, Macho, Masikio, Pua, Kuwepo katika sehemu fulani n.k, kwa sababu yeye yupo kabla ya kuwepo kitu chochote, na yeye hahitaji kitu, Sifa zake za Dhati ni yeye mwenyewe, anajua kwa Dhati yake, Anaweza kwa Dhati yake, Anasikia kwa Dhati yake, kwa maana Dhati yake imekamilika haihitaji kitu chengine katika kusifika, Uhai wake ni wakidhati, Usikuvu wake ni wakidhati, Uoni wake ni wakidhati, Elimu yake ni yakidhati, Uwezo wake ni wakidhati, na namna hivi.

Ø  Kuitakidi Usamehevu bila ya Toba: Mayahudi na Manasara walisema kua Pepo ni kwa ajili yao tu, na kua wao hata kama wataadhibiwa basi ni kwa Muda mdogo wa siku chache tu, kisha watasamehewa na kwenda Peponi, haya anayaeleza Allah katika kitabu chake, na kueka wazi, kua ndio yaliyowapeleka katika kudharau Mafundisho ya Allah, na kuyageuza ili yakubaliane na Mapendwa Moyo yao, na kuiharibu Dini kwa kujichukulia Pato la kidunia, kisha wao Watasamehewa tu. Basi tujue kua haya ndio Maradhi mabaya kabisa kwa waliopita, na ujihadhari yasije yakapata Nafasi katika Fikra zako, kua na wewe maadamu ni Muislamu utafika Peponi tu, hata kama utaadhibiwa basi ni kwa Muda tu, ukawa huna tofauti na hao waliopita kabla yetu isipokua Majina tu, na ujue kua Allah ameiandaa Pepo kwa ajili ya Waja wake walio Wachamungu Waumini waliowema, na kua Allah ameandaa Adhabu ya Moto kwa ajili ya Waja wake Waovu wenye kumuasi wote, ambao wameondoka na hawakutubia, basi na wewe ukiwa umo katika kosa Kubwa, na hutubii ujijue kua Pepo ni haramu juu yako, na wala kutokosekana katika Moto milele; basi tujiandae na sio kujipa matamanio tu, tukawa kama hao waliopita.

Ø   Uislamu unahifadhi: mambo matano ya Dharura katika Uhai; Dini, Akili, Nafsi, Heshima na Mali.

1.      Dini: inahakikisha Utulivu wenye malengo ya Kuridhiwa na Mola wako -aliyeumba kila kitu- katika Maisha yako, basi ni lazima kulinda Dini kwa Nafsi, Mali, Fikra, Malezi na Wakati.

2.      Akili: Ni Haramu katika Uislamu kila linaloharibu Akili, k.m: Ulevi; Ni lazima kuilinda na kila linaloharibu Akili, na kuihifadhi kwa kuikuza.

3.      Nafsi: nayo ni mwili, ni Haramu yanayosababisha kuiangamiza nafsi bila ya Haki, kama vile kijiua, kuua, kuvuta Sigereti. Ni lazima kuuhifadhi Kiafya, Chakula bora, na Usafi.

4.      Heshima: Kila ninaloharibu heshima ya Muislamu ni Haramu, kama Matusi, Uzinifu, kutembea Uchi; ni lazima kulinda Heshima zetu kwa Malezi bora ya Kiislamu, na kukaa mbali na kila linalovunja na kuhatarisha Heshima zetu.

5.      Mali: ya Muisalmu ni Haramu isipokua kwa kuridhika mwenyewe, na katika anayoridhia Allah Mtukufu; ama wizi, dhulma, rushwa, riba, kamari, shahada za Uongo vyote hivi ni Haramu.

Ndugu yangu huu ndio Uislamu kama ulivyo katika kitabu cha Allah Qur-ani, na Mafundisho sahihi yanayotoka kwa Mtume Muhammad (s.a.w), na yasiyodhurika na mwenye kwenda kinyume nayo, au kuyawacha, na kila Moja katika haya lina Ushahidi wa Kutosha katika Kitabu cha Allah.

Assante sana.

Wassalamu alaykum warahmatullahi

wabarakatuh.

B

Ndugu yako: Hafidh. H. Seif Sawafiy

Imamu Msikiti wa Ibadhi - Bujumbura

sawafiy@yahoo.com

Box 17 Chake Pemba Tanzania

Tunakutakia usomaji mwema

(Amin).

1426A.H-2005A.D

 

Copyright ©2005  Uislam.net