CHEO CHA MTUME MUHAMMAD (S.A.W)

Bismillahi Rrahmani Rrahim. Baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu na kumtakiya rehma Bwana Mtume wetu Muhammad Salla Llahu Alayhi Wasalam na Masahaba zake wote.

Shukurani zote ni kwa ALLAH mtukufu, na Rehma na Amani ziwe kwa Mbora wa viumbe Mtume wetu Muhammad (s.a.w) pamoja na Aali zake na Maswahaba wake na kila mfuasi wa Uadilifu wake mpaka siku ya malipo (Amin).

Kwa hakika ALLAH  mtukufu anamnyanyua katika Daraja anayemtaka miongoni mwa Viumbe wake, basi amemtukuza na kumnyanyua daraja ya juu kabisa Mtume wetu Muhammad (s.a.w), ni fadhila anaiweka ALLAH  mtukufu kwa anayemtaka. Amesema Mtume Muhammad (s.a.w): Mimi ni mbora wa watoto wa Adam wala hakuna Fakhari" na anasema: Lau kua Ndugu yangu Mussa yuko hai basi asingalipata nafasi isipokua ya kunifuata mimi"; inatosha kua ALLAH  Mtukufu hakumukhutubia kwa jina lake lakini kwa Cheo chake, tafauti na Mitume mengine -juu yao iko Rehma na Amani-, na akamsifu kua ni Rehma kwa ajili ya Walimwengu wote: Wala hatujakutuma isipokua ni Rehma kwa Walimwengu" vile vile amekhusishwa na ALLAH  kwa safari maalumu ya kufika mbinguni katika Usiku maalumu wa Miijar, hiyo ilikua ni zawadi ya kumpeleka katika sehemu yenye cheo cha kukifikwa yeye (s.a.w) ambacho hajakipata yeyote katika waliopita kabla yake, nacho ni Daraja ya kua Mtume wetu Muhammad (s.a.w) ni Imamu, na Manabii wote wako nyuma yake wakiongozwa na yeye. Pia ALLAH  Mtukufu ameufanya Umma wa Muhammad (s.a.w) kua ndio Umma bora kabisa baina ya Umma zote zilizopita: Mumekua Umma bora uliotolewa kwa ajili ya Watu" na kesho Akhera ALLAH  mtukufu atamnyanyua Daraja Mtume wake Muhammad (s.a.w) kwa kumfanya kua ni Muombezi wa watu wote katika kuanza Hesabu na Kuingia katika Pepo zilizoandaliwa: Ili akunyanyue Mola wako Sehemu ya Kutukuzwa".

  Na sisi tukiwa tumo katika kumbukumbu za kuzaliwa Mtume wetu Muhammad (s.a.w) hatuna budi kueleza kua ALLAH mtukufu amejaalia Umma huu uwe ni Umma wa kati na kati, na kututaka -ALLAH- tuwe sisi ni wenye matarajio kwa kuzipita sababu zake, na kama kawaida ALLAH mtukufu anatuelezea Umma zilizopita kabla yetu ili tusije tukafuata nyayo zao, na miongoni mwa nyayo zao zilizoelezewa katika Kitabu ni kupindukia katika Mipaka katika Dini, Wakiristo wamepindukia mipaka katika cheo cha Mtume Issa bin Marayam (a.s.w) hata wakamfanya kua ni Mungu, na wengine wakafanya kua ni Mtoto wa Mungu, na kua yeye ni mmoja katika utatu, na Mayahudi wakapindukia mipaka yao mpaka wakamfanya Uzairi kua ni Mtoto wa Mungu, na Wakawafanya watukufu wao ni Mabwana wakamsahau ALLAH.

Yote hayo yameelezwa katika Qur-ani ili tuzingatie tusije tukapindukia Mipaka ndani na Dini hasa katika Haki ya Mtume wetu Muhammad (s.a.w); lakini Jee!! Tumezingatia katika hilo la kupindukia mipaka katika Haki yake au tumalivamia?

Kwa hakika tumevuuka Mipaka katika Haki ya Mtume wetu Muhammad (s.a.w), na hayo yako wazi katika Mambo yafuatayo:-

1.    Shafaa ya Mtume (s.a.w): Kuitakidi kwetu kua Mtume (s.a.w) atakuja kuwaombea Waislamu wote waliokufa hali ya kua wameyavaa Madhambi makubwa yasiyokua ya Kishirikina ni jambo linalokwenda kinyume kabisa ya yaliyokuja katika Qur-ani, kwa sababu Qur-ani inatubainishia kwa Uwazi kabisa kua Madhalimu hawatopata Uwombezi wala Rafiki: Hakuna kwa Madhalimu fariki yoyote wala muombezi wa kutiiwa" na Udhalimu katika Sharia ya ALLAH  mtukufu unakusanya kila kosa kubwa, kwa hivyo mwenye kwenda kwa ALLAH na yeye anao mzigo wa Kosa kubwa huyo anayo sifa hiyo ya Udhalimu ajijue kua hana Uwombezi wala Rafiki. Na vipi apate uwombezi au Rafiki hali ya kua yeye yumo katika hali ya Ufasiki, na fasiki haridhiwi mbele ya ALLAH mtukufu: Basi ikiwa mutaridhia kwao; basi kwa hakika ALLAH  haridhii watu mafasiki". Hakika kuishi kwa Muislamu katika Maisha haya na huku amebeba Fikra ya kua yeye hatodhurika na Maasi kwa sababu ya Mtume wake Muhammad (s.a.w) ni kupindukia Mipaka (Ghuluwu) katika Dini. Naam Shafaa ya Mtume (s.a.w) ipo lakini Shafaa hiyo inawakusanya Waumini walio safi kotokana na makosa, wametubia kabla ya kuondoka hapa Duniani, hao ni Wachamungu, hawa peke yao ndio wenye Haki na Shafaa ya Mtume (s.a.w) kwa kupandishwa Daraja zao katika Pepo, na kufanyiwa haraka hesabu zao, na kukubaliwa Toba zao, na kuwekwa mbali na Mabayaya waliyoyafanya kasha wakatubia, kama ilivyokuja katika Surati Ghaafir: Ambao wanachukua Arshi na walio pembezoni mwake wanatukuza kwa utukuzo wa Mola wao na wanamuamini yeye na wanaomba msamaha kwa ajili ya walioamini; Mola wetu umekienea kila kitu kwa Rehma na Elimu; basi samehe kwa wale ambao wametubia na wakafuata njia yako na uwaepushie Adhabu ya Moto *  Mola wetu; na uwaingize katika Pepo safi ambayo umewaahidi, na aliyetengenea katika Baba zao na Wake zao na Vizazi vyao; Hakika yako wewe ni Mwenye nguvu Mwenye hikima *  Na uwaepushie Mabaya, na ambaye unamuepushia Mabaya siku hiyo basi umemrehemu; na hayo ndio Mafanikio Makuu" Basi tujihadhari na yale ya Batili yaliyozuliwa katika Haki ya Mtume wetu Muhammad (s.a.w), ambayo yanamjenga anayeyakubali katika matarajio ya Uongo yasiyokua na Ahadi katika Kitabu cha ALLAH, na yenye kwenda kinyume na Qur-ani.

2.    Kutoka Motoni: Katika mambo yaliyopo -nayo ni kupindukia Mipaka katika Haki ya Mtume wetu Muhammad (s.a.w)- ni kule kuitakidi kwetu kua yeye hatoacha kwenda katika Moto wa Jahannam ili kuwatoa Waislamu waliomo humo, mpaka wamalizike wote, ni Itikadi inayokwenda kinyume kabisa na Kitabu cha ALLAH Mtukufu, kwa sababu kitabu cha ALLAH  kinatuwekea Bayana ya wazi, kua hakuna kutoka katika Moto milele; kwa atakayeingia humo ataendelea ni kubakia bila ya kukosekana: Hakika Wema watakua katika Neema *  Na hakika Waovu watakua katika Moto mkali *  Wataufikia siku ya Malipo * Na haitokua kwao na huo wenye kukosekana" Sasa vipi yanatufikia Mafundisho kua Waovu watatolewa Motoni si uongo ni nini? Na hali ya kua hakuna hata Aya moja inayoeleza kua kuna Mtu atatoka Motoni, basi Qur-ani inatueleza kua Itikadi hii ni katika Kupindukia Mipaka ndani ya Dini: Basi Ole wao ambao wanaandika Kitabu kwa mikono yao kisha wanasema: Haya ni kutoka kwa Allah" ili wanunue kwa hayo thamani ndogo; Basi ole wao kwa hayo iliyoandika Mikono yao; na ole wao kwa hayo waliochuma * Na wamesema: Hautotugusa Moto isipokua siku zenye kuhesabika" Sema: Jee!! Mulichuka kwa ALLAH Ahadi; basi hatoiendea kinyume ALLAH Ahadi yake; au munasema juu ya ALLAH yale musiyoyajua?"

3.   Kumuabudu Mtume (s.a.w): Na hili ninaingia kwa wale Wajinga wanaojinasibisha na Uislamu, wao wamepindukia Mipaka mpaka kumfanya Mtume (s.a.w) kua ni kama Mungu wa Kuombwa, hali ya kua ALLAH  Mtukufu amesema: Hakika Misikiti ni ya ALLAH  basi usiombe pamoja na ALLAH  yoyote" Aya iliyokua wazi kabisa kua yeye ALLAH hataki ushirikisho katika Dua, lakini utawakuta wengine baada ya kumuelekea ALLAH  mtukufu wanamuelekea Mtume (s.a.w) na wanamuomba yeye, na hapa sikusudii Tawassuli inayokubalika ndani ya Sheria, nayo ni kumuomba ALLAH Mtukufu kwa kumtaja Mtume (s.a.w) kua yeye ni Haki na Rehma, kwa mfano: Ewe Mola kwa Haki ya Mtume wako Muhammad (s.a.w) tuwezeshe tuwe Wachaungu" huku ni kumuomba ALLAH  mtukufu na sio Mtume (s.a.w) ifahamike vizuri, na Haki ya Mtume (s.a.w) ni ule Uongofu wake wa Haki, kwa hivyo ni kutuwezesha kuifuata Sheria yake na Uongofu wake ili tuwe Wachamungu; ama kulikusudia kaburi lake kwa kwenda kumlilia Mtume (s.a.w) na huku unamuomba na kuyayatika, ni mambo maovu katika Uislamu nayo ni katika mila za Kishirikina.

4.   Kuvuka mipaka katika cheo chake: Na haya ni Maradhi waliyonayo baadhi ya Watu, kiasi cha kua akiambiwa kua ALLAH amesema kitu Fulani, na maneno ya Qur-ani yako mbele yake anayaona; unamuona anayachuka maneno ya ALLAH  kua ni jambo la kawaida, na kuyarudi kwa Mapokezi ya Dhana kua Mtume ameyasema, na kuyapa mapokezi hayo cheo kikubwa zaidi kuliko maneno ya ALLAH mtukufu, ni maradhi mabaya kabisa, nako ni kuvuuka mipaka katika Haki ya Mtume (s.a.w), kwa sababu Qur-ani ndio Hakimu wa juu kabisa, na yeye sio wa kuhukumiwa, na yako Mengi ya Uzushi ambayo yalifanywa na Wajinga dhidi ya Mtume (s.a.w); na hili ndio lililowaingiza baadhi ya Wajinga katika kunyanyua vyeo vya Wanachuoni wao kuliko Vyeo vya ALLAH  na Mtume wake (s.a.w) na kusema: Hakuna kheri katika Kitabu cha ALLAH bila ya Sunna; wala hakuna kheri katika Sunna bila ya ufahamu wa Wema wetu waliotangulia" na wengine hawalisemi hilo kwa ulimi wa maneno, lakini kwa ulimi wa hali zao. Na hawa zimegeuka Mezani kwao, ALLAH atuondoshee kila fitna, na atujaalia katika anayoyaridhia. Na hili halina maana ya kua ni kudharau Mapokezi na Juhudi za Wapokezi lakini ni kuilinda Dini na Uchafuzi wa wachafuzi, na yaliyosahihi katika Mapokezi yanakubaliwa na yanafanyiwa kazi lakini kwa Mezani ya Ushahidi; kwa sababu Mtume (s.a.w) hawezi kwenda kinyume na Kitabu cha Qur-ani, kwani Mwenendo wake (s.a.w) ni Sheria kwa mujibu wa Qur-ani, na hapa itakua matokeo yake ni kuivunja Qur-ani, na ndio ALLAH akasema: Na lau atajisemea juu yetu baadi ya Majineno *  Kwa hakika tungalichukua kwake kwa Nguvu * Kisha kwa hakika tungalikata kwake mshipa wa shingo *  Basi hakuna yeyote katika nyinyi kua kwake wazuizi" sasa vipi aseme au afanye au aridhie kinyume na Qur-ani? Na ndio yakapokewa Mapokezi Sahihi kutoka kwake (s.a.w) kua amesema: Hakika nyinyi mutatofautiana baada yangu; basi kitakachokuja kwenu kutoka kwangu kiwekeni katika Kitabu cha ALLAH; basi kitakachukubaliana nacho hicho kinatoka kwangu; na kitakachopingana nacho hicho hakitoki kwangu" sasa kimebakia kile ambacho hakipingani na Qur-ani wala hakimo katika Qur-ani, hicho kitakua katika Uhakikisho zaidi wa Wanavyuoni, kwa sababu ALLAH mtukufu amesema: Basi waulizeni Wana kumbukumbu ikiwa nyinyi hamujui * Kwa Ubainisho na Dalili.. .

5.   Kutukuza Watu wa mezani ya Mtume (s.a.w): Wako wengine wamejiingiza katika kuzingatia Usharifu katika Dini ni sawa Usharifu wa Kisuhuba au wa Kiukoo, na wengine wamepindukia mipaka zaidi katika Jamaa wa Mtume Muhammad (s.a.w), hata ikafikia kwao kuwapa urithi wa Sheria, na kuwapa Taathira katika Uhai, ni upotevu juu ya Upotevu, kwa hakika Dini ya Uislamu haikuja kumnyanua mtu kwa sababu ya Ukoo wake, wala Utaifa wake, wala Ukabila wake, wala Usuhuba wake, lakini Uislamu umekuja katika mezani ya Uadilifu, ya kua watu wote ni Sawa mbele ya ALLAH  mtukufu amesema ALLAH  mtukufu: Enyi watu,, Hakika sisi tumekuumbeni kutokana na mwanamume na mwanamuke, na tumekujaalieni Mataifa na Makabila ili mujuane; Hakika Mbora wenu kwa ALLAH  ni Mchamungu wenu zaidi; hakika ALLAH  ni Mjuzi Mwenye khabari" kwa hivyo Mezani ya Uadilifu mbele ya ALLAH  ni Uchamungu, na sio chengine chochote, basi amesema ALLAH: Hakika ayakubali ALLAH kutoka kwa Wachamungu" na Baba wa Mtume Ibrahimu (a.s.w) ni Mtu wa Motoni milele kwa Ubainisho wa Qur-ani, na Mtoto wa Mtume Nuuh (a.s.w) ni wa Motoni milele kwa ubainisho wa Qur-ani, na Mke wa Mtume Nuuh na Mtume Luut (a.s.w) -wake wao wote- ni Motoni milele kwa Maelezo ya Qur-ani, na waliokufuru katika Bani Israaili -juu ya kua wao ni wato wa Manabii- wamelaaniwa katika Ulimi wa Dauni na Issa mwana wa Mariyamu (a.s.w): hayo ni kwa sababu ya kule Kuasi kwao na walikua wakifanya Uadui" kwa ubainisho wa Qur-ani, na katika yaliyopokewa kutoka kwa Mtume wetu Muhammad (s.a.w) aliwaambia watu wake wa Karibu akiwemo Bibi Faatimah (r.a): ..Ifahamike ya kua Vipenzi wangu katika nyinyi ni Wachamungu, wasije wakaja watu siku ya Kiama na Dini, na nyinyi mukanijia na Dunia mumeichukua…" hiyo ndio Mezani ya Usawa kwa ajili ya Watu wote, sasa vipi tena yaje mambo ya Kurithi kwa kutumia Nasabu? Hali ya kua Qur-ani inatubainishia kua Kuangalia Asili ni sababu ya Kibri, pale aliposema ALLAH akituelezea aliyoyasema Ibliisi Mal-uuni: Mimi ni bora kuliko yeye umaniumba kutokana na Moto na umemuumba kutokana na Dongo" aliangalia Asili yake akadharau Amri ya Mola wake.

Tunamuomba ALLAH mtukufu atuwezeshe katika anayoyaridhia na atuepushe na anayoyakasirikia tuwe sababu ya Uongofu tusiwe Wapotovu wala Wapotevu. Na anyanyue Bendera ya Waumini na aangushe Bendera ya Makafiri, na awaondoshee ndugu zetu Udhalilifu popote pale walipo, na aunganishe nyoyo za Vijana katika Utiifu wake. Na Rehma na Amani ziwe kwa Aliyechaguliwa Mtume wetu Muhammad (s.a.w) pamoja na Aali zake na Maswahaba wake mpaka siku ya Malipo .

(Amin).

Wassalamu alaykum warahmatullahi wabarakatuh

Ndugu yenu: Hafidh. H. Seif Sawafiy

Imamu wa Msikiti wa Ibadhi Bujumbura – Burundi.

sawafiy@yahoo.com

09/03/1426H – 18/04/2005M

Copyright ©2005  Uislam.net